Ronaldo wa Brazili Abambikiwa Mtoto

Thursday, September 24, 2009 / Posted by ishak /


Nyota wa Brazili, Ronaldo de Lima ametakiwa na mahakama nchini Brazili afanye vipimo vya DNA ili kuondoa mzozo wa kubambikiwa mtoto na mwanamke raia wa Brazili anayeishi nchini Singapore.
Tangia Ronaldo aliporudi Brazili mwaka 2008 toka timu ya AC Milan ya Italia, amekuwa akikumbwa na maskendo mbali mbali kama vile kuanikwa kwenye magazeti baada ya kulala na mashoga hotelini na kisha kukataa kuwalipa baada ya huduma.

Safari hii Ronaldo amekumbwa na skendo jingine akidaiwa kuzaa na mwanamke raia wa Brazili anayeishi nchini Singapore na kisha kumkataa mtoto wake.

Ronaldo ambaye hivi sasa anaichezea timu kongwe ya Brazili ya Corinthians ametakiwa na mahakama nchini humo kufanya vipimo vya DNA ili kumaliza mzozo wa mwanamke anayedai Ronaldo ni baba wa mtoto wake mwenye umri wa miaka minne.

Taarifa toka jiji la Rio de Janeiro zinasema kwamba mwanamke huyo anayejulikana kama Michele Umrazu mwenye umri wa miaka 27, awali kabla ya kudai amezaa na Ronaldo alikuwa akidhania mtoto wake mwenye umri wa miaka minne ni wa mpenzi wake wa zamani raia wa Marekani.

Lakini baada ya vipimo vya DNA kufanyika na kugundulika kuwa mtoto huyo si wa huyo Mmarekani, Michele aligeuza kibao na kudai kuwa mtoto huyo ni wa Ronaldo.

"Nywele zake, macho yake mpaka pua vyote vinafanana na Ronaldo" alisema Michele.

Mama yake Michele alidai kwamba Ronaldo ambaye aliwahi kuchaguliwa kuwa mchezaji bora wa dunia mara tatu, alikutana na Michele kwa mara ya kwanza mwaka 2002 wakati wa kombe la dunia nchini Japan.

Walikutana tena mwezi wa nane mwaka 2004 ikiwa ni miezi tisa kabla ya kujifungua mtoto huyo.

Kutokana na Ronaldo kumkataa mtoto huyo, mzozo ulifika mahakamani na sasa mahakama imemtaka Ronaldo afanye vipimo vya DNA ili kumaliza mzozo huo.

Ronaldo ambaye alitimiza miaka 33 siku mbili zilizopita ana watoto wengine wawili Ronald, mwenye umri wa miaka tisa na Maria Sofia mwenye umri wa miezi tisa.

Ronaldo alithibitisha mwezi uliopita kuwa anatarajia mtoto wa tatu mwanzoni mwa mwaka ujao.

source.nifahamishe.com

0 comments:

Post a Comment