Pinda atangaza mali zake

Friday, January 15, 2010 / Posted by ishak /


WAZIRI Mkuu wa Tanzania, Mizengo Pinda ametangaza mali zake alizonazo anazozimiliki mbele ya vyombo vya habari ofisini kwake jana.
Pinda alitangaza mali hizo zikiwemo na shilingi milioni 25 kwenye akaunti yake, nyumba tatu za kawaida moja ikiwa jijini Dar es Salaam, Mpanda na Dodoma na gari moja alilolinunua kwa mkopo.

Waziri Pinda aliamua kufanya hivyo ili kuweka bayana mali zake na kuonyesha mfano kwa viongozi wote nchini kufata kwa kuwa viongozi walitakiwa kuweka bayana mali zao ili kutekeleza sheria ya maadili ya uongozi.

"Hizo ndizo mali zangu nilizo nazo ndugu" alisema mbunge huyo wa Mpanda wakati akitangaza mali zake

Waziri mkuu aliyetambulika kwa jina la mtoto wa mkulima alitaja mali zake hizo na kusema haelewi yeye kwake utajiri ni nini na kusema mali hizo kwake anajiona ni tayari zimeshamtosheleza na wakati akianza kutaja mali zake hizo wka kujielezea mbele za wahariri alianza kwa kusema

"Nina nyumba Dodoma kutokana na utaratibu wa mikopo ya nyumba za serikali; nina nyumba Mpanda ambayo imepatikana kwa mpango wa kawaida tu, imetokana na visenti kidogo nikanunua pale ambapo bahati nzuri gharama za ujenzi hazikuwa kubwa sana, nikakikarabati kipo pale kipo Makanyagio pale."

"Haya! Ukitoka pale unataka niseme nini tena. Dar es Salaam sina nyumba ya kusema ya maana sana ukienda shambani Pugu kule kipo kinyumba kidogo hivyo inahitajika kazi ya ziada kuweza kufanya paonekane pa maana.

"Kijijini kwa baba yangu pale Kibaoni sina nyumba; pale mlipoona nimekaa na bibi tunapiga porojo, kile kijumba mimi na wadogo zangu tulimsaidia babu kwa ajili ya kumjengea babu yetu na pale ndipo nilipokuwa nafikia siku zote wakati wa likizo."

Pinda, ambaye amekuwa mbunge tangu mwaka 2000, alisema miaka yote alikuwa akifikia kwenye nyumba hiyo ambayo yeye ana chumba chake kimoja hali kadhalika babu yake.

Alisema baada ya kuteuliwa kuwa waziri mkuu, alijikuta kwenye wakati mgumu sana kwa kuwa alitaka kuendelea kufikia kwenye nyumba hiyo, lakini watu wa usalama walimkataza.

"Baada ya hii maneno inayoitwa uwaziri mkuu, nilipoteuliwa nikataka nifikie pale katika ile nyumba, lakini nikaambiwa hapana; haiwezekani; hapafai; huwezi kufikia pale,"alisema.
Alisema hilo ndilo lilikuwa tatizo lake la kwanza kwa hiyo anajaribu kujenga tena kitu ambacho na yeye atapata mahala pa kufikia pamoja na wasaidizi wake kwenye eneo hilo.

"Nimegundua tatizo ni hawa wakubwa. Pale kijijini kwetu hakuna nyumba za wageni hatuna chochote mi nilidhani nikienda kule nikiachwa kwa babu na bibi, wao wataenda huko umbali wa kilomita wakatafute pa kupumzika, lakini wakasema no! no! no! haiwezekani, nikawaelewa," alisema.

Alisema ukiondoa nyumba hiyo, vitu vya maana zaidi hana labda gari la mkopo na ni gari la mbunge.
Pinda aliendelea kuwaambia wahariri kuwa

"Hivi ukifika hivi unahitaji nini cha zaidi tena? Kwa hiyo kipato kidogo unachokipata unaweza kukitumia kwa ajili ya huduma za watoto wako kusoma na kadhalika kwa sababu ni vitu viko nje ya taratibu za serikali. Kwa hiyo huwa najiona tu kwamba na mimi nina bahati tu kwamba Mungu alinifikisha hapa nilipofika na kunifikisha katika nafasi hii imenipa ahueni," alisema.

Alisema kama masuala hayo muhimu yanatimia, wajibu wake ni kujaribu kulipa fadhila kwa Watanzania kwa kufanya kila atakaloweza kuwatumikia vizuri zaidi.

"Kwa hiyo mimi nina hakika zaidi kuwa kwa nafasi kama niliyo nayo, naweza kuishi bila tamaa ya mambo mengine zaidi... mimi hata hisa sina, sijanunua hisa mahali popote, lakini huko tunakokwenda naweza nikatamani nikatafuta hata hisa hivi, kwa ajili labda ya sababu fulani fulani," alisema.


SOURCE.NIFAHAMISHE

0 comments:

Post a Comment