Safari ya Kuzamia Italia Ndani ya Begi.

Wednesday, January 20, 2010 / Posted by ishak /


Raia wa Afghanistan mwenye umri wa miaka 15 amenaswa na maafisa wa uhamiaji wa Italia akizamia nchini humo akiwa amejificha ndani ya begi.
Maafisa wa uhamiaji wa Italia walipigwa na butwaa baada ya kulisimamisha gari dogo aina ya Peugeot 207 na kumkuta kijana wa Kiafghanistan mwenye umri wa miaka 15 akiwa amejificha ndani ya begi lililokuwa limewekwa kwenye buti la gari hilo.

Raia wa Ugiriki Alexandros Lepesiotis, 42, aliyekuwa akiliendesha gari hilo anashikiliwa na polisi kwa makosa ya kujaribu kuwaingiza kinyemela nchini Italia, kijana huyo na kaka yake mwenye umri wa miaka 17 ambaye naye alikutwa kwenye buti la gari hilo akiwa amefunikwa na mablanketi.

Polisi walilisimamisha gari la Lepesiotis katika taratibu za kawaida za polisi za kukagua magari yanayoingia Italia toka Ugiriki lakini walishangazwa na jinsi Lepesiotis alivyokuwa akionyesha wasiwasi gari lake lilipoanza kukaguliwa.

Taarifa zilisema kuwa vijana hao wa Kiafghanistan walimlipa dereva huyo wa Kigiriki euro 2600 ili awaingize kinyemela nchini Italia.

Vijana hao walipata pesa hizo kutokana na kazi za kuosha vyombo kwenye migahawa ya Ugiriki.

Vijana hao wamehifadhiwa katika mji wa Bari nchini Italia wakati taratibu za kuwasiliana na wazazi wao zikifanyika na pia kuangalia kama wapewe haki ya ukimbizi au la.

source nifahamishe

0 comments:

Post a Comment