Oh Mapenzi Kweli Yanachanganya Akili!

Saturday, February 20, 2010 / Posted by ishak /


Oh mapenzi mapenzi, wakati mwingine mapenzi hutufanya tufanye mambo mengi ya ajabu tusiyotarajia kuyafanya, mapenzi hayo hayo ndiyo yaliyomfanya mwanaume mmoja wa nchini Ujerumani awe anaruka ukuta kuingia jela kumfuata mpenzi wake aliyetupwa jela, alifanya hivyo si mara moja ni kila siku usiku mpaka siku aliponaswa akiruka ukuta.
Mwanaume huyo mwenye umri wa miaka 33 wa mji wa Bielefeld nchini Ujerumani aliyetambulika kwa jina la Daniele E. alijikuta na yeye akitupwa jela kwa kosa la kuruka ukuta na kuingia jela.

Kwa mujibu wa gazeti la kila siku la mji huo Westfalen-Blatt, Daniele amepatikana na hatia ya kuzamia jela na kesi yake itaanza kusikilizwa mwezi ujao.

Taarifa zilisema kuwa Daniele alikuwa akiruka ukuta kila siku usiku kuingia kwenye jela ya wanawake yenye ulinzi mdogo ili kumfuata mpenzi wake aliyetupwa jela baada ya kukamatwa na madawa ya kulevya.

Daniele alisema kuwa alikuwa anashindwa kuishi mbali na mpenzi wake aliyesema alimvalisha pete ya uchumba kabla ya kukamatwa na kutupwa jela.

Mambo yalikuwa moto moto kwenye selo namba 13 ya jela hiyo ambayo haikutajwa jina, Daniele alisababisha kero kwa wafungwa wengine wanawake kutokana na kelele za mapenzi walizokuwa wakizitoa usiku yeye na mpenzi wake.

Baadhi ya wafungwa wanawake walilamika kuwa Daniele alikuwa akiwakosesha usingizi huku wafungwa wengine wakiwa na matumaini siku moja Daniele atawatimizia na wao hamu zao za kimapenzi.

Baada ya malalamiko kufikishwa kwa maafisa wa jela hiyo, kamera za ulinzi ziliwekwa kuzunguka ukuta wa jela hiyo na ndipo novemba 8 mwaka jana Daniele aliponaswa akiruka ukuta kuingia kwenye jela hiyo.

Daniele alitupwa jela ya wanaume akisubiri hukumu ya kesi hiyo pamoja na kesi zingine za kupora pesa kwenye vituo kadhaa vya mafuta zilizogundulika baada ya kukamatwa kwake.

Kwa mujibu wa sheria za jela hiyo, Daniele na mpenzi wake wangeweza kupewa ruhusa ya kutembeleana mara kwa mara ili kuokoa uhusiano wao lakini tatizo ni kwamba mpenzi wa Daniele aliandika jina la mwanaume mwingine kama mpenzi wake siku aliyotupwa jela kutumikia kifungo chake.

source nifahamishe

0 comments:

Post a Comment