Sinema ya Kutisha Yasababisha Watu Wakimbizwe Hospitali

Saturday, February 13, 2010 / Posted by ishak /


Sinema ya kutisha ya 'Paranormal Activity' imezua kasheshe nchini Italia baada ya msichana mmoja kupooza mwili wake na watu wengi walioiangalia filamu hiyo kuwahishwa hospitali wakiwa hawajitambui.
Filamu hiyo iliingia kwenye kumbi za sinema za Italia bila kuwekwa katika fungu lolote la umri tofauti na Marekani ambako iliwekwa katika fungu la watu wazima "R" na nchini Uingereza ambako watu wenye umri chini ya miaka 15 hawakutakiwa kuiangalia filamu hiyo.

Hivi sasa kuna shinikizo kubwa nchini Italia wazazi wakitaka filamu hiyo ionyweshwe kwa watu wenye umri zaidi ya miaka 18 pekee.

Kwa jinsi filamu hiyo ilivyofanikiwa kuwatisha watu wengi, huduma za dharura za hospitali nchini Italia ziliwapokea mamia ya watu walioiangalia filamu hiyo siku ya jumamosi ambao walishindwa kujitambua kutokana na kupaniki.

Hata tangazo la filamu hiyo linadaiwa kuwatisha maelfu ya watoto lilipoonyeshwa kwenye televisheni za Italia.

Hali ilikuwa mbaya zaidi kwa msichana mmoja mwenye umri wa miaka 14 ambaye aliwahishwa hospitali akiwa amepooza mwili wake baada ya kuangalia filamu hiyo.

Hata waziri wa ulinzi wa Italia, Ignazio La Russa, ameingia kwenye zogo la filamu hiyo akisema kuwa kwa wiki mbili tangazo la filamu hiyo limekuwa likiwatisha sana watoto linapoonyeshwa mara kwa mara kwenye televisheni za Italia.

"Inatisha kweli, nakumbuka wakati mtoto wangu wa kiume wa miaka saba aliponiambia "Baba Naogopa" alipoona tangazo la filamu hii", alisema waziri huyo wa ulinzi.

Filamu ya Paranormal Activity ilitengenezwa kienyeji kwenye nyumba ya
mtayarishaji wake Mmarekani Oren Peli. Sinema hiyo iligharimu dola 15,000 tu tofauti na filamu za Hollywood ambazo hugharimu mamilioni ya dola.

Hata hivyo ilipoingia kwenye kumbi za sinema nchini Marekani mwezi oktoba mwaka jana ilifanikiwa kuingiza dola milioni 22 ndani ya wiki moja.

source nifahamishe

0 comments:

Post a Comment