Mugabe Kugombea Urais Kwa Mara Nyingine

Friday, March 05, 2010 / Posted by ishak /


Rais wa Zimbabwe, Robert Mugabe ambaye hivi sasa ana umri wa miaka 86 amesema yuko tayari kugombea urais kwa mara nyingine kuliongoza taifa la Zimbabwe.
Akiongea na waandishi wa habari mjini Harare, rais Robert Mugabe ambaye anaendelea kuiongoza Zimbabwe kwa miaka 30 sasa, alisema kuwa yuko tayari kugombea tena urais kwenye uchaguzi mkuu utakaofanyika miaka miwili ijayo.

Mugabe alisema kuwa iwapo chama chake cha ZANU-PF kitampitisha kugombea urais basi atasimama kwa mara nyingine kugombea urais.

Mugabe ambaye alianza kuitawala Zimbabwe tangia ilipopewa uhuru wake kutoka kwa Waingereza mwaka 1980, alishinda uchaguzi wa urais uliopita ingawa kambi ya upinzani iligoma kukubali matokeo ya uchaguzi ikisema kuwa hila zilifanyika.

Hali hiyo ilisababisha mtafaruku nchini Zimbabwe ambapo uchumi wake uliyumba kutokana na vikwazo vya kiuchumi vilivyowekwa na mataifa ya magharibi.

Pesa ya Zimbabwe ilipoteza thamani yake na kuifanya Zimbabwe izitose pesa zake na kuanza kutumia dola za kimarekani na Rand za Afrika Kusini kama mbadala wa pesa zake.

source nifahamishe

0 comments:

Post a Comment