Fundi Apoteza Maisha Baada ya Kuanguka Toka Ghorofa ya Nne

Wednesday, May 12, 2010 / Posted by ishak /

MWANAUME mmoja aliyetambulika kwa jina la Msepele Salum, mkazi wa Kigamboni, amefariki dunia mara baada ya kuanguka kutoka ghorofa ya nne wakati akiwa katika shughuli za ujenzi maeneo ya katikati ya jiji.
Tukio hilo lilitokea jana majira ya mchana, katika makutano ya barabara ya Indiragand na Bridge wakati akiwa katika ujenzi wa ghorofa mali ya shirika la nyumba la Taifa.

Mashuhuda waliokuwa eneo la tukio ambao ni mafundi wenzake walidai kuwa, marehemu alikuwa akiendelea na ujenzi katika ghorofa ya nne ambapo yeye alikuwa ni fundi wa kujenga na wengine walikuwa ni mafundi rangi na mafundi wengine wa aina mbalimbali.

WAlisema kuwa wao wakiwa katika gorofa ya tatu walisikia kishindo kikubwa chini na walidharau na kuendelea na shughuli zao, ndipo mmoja wao alipoamua kushuka chini na kumkuta mwenzao huyo ameanguka chini na alikuwa tayari ameshakufa.

Ndipo walipotoa taarifa kituo cha polisi na maafisa wa polisi kuja kupima eneo hilo ili kuthibitisha kifo cha marehemu huyo, na wakati wakiwa katika upimaji huo marehemu aligundulika alifariki papohapo kwa kuwa alipoanguka kichwa chake kilipasuka.

Hata hivyo katika uchunguzi wa kina ulibainika kuwa mafundi hao walikuwa wakiendela na shughuli za ujenzi bila ya kuwa na vifaa maalum vya kuwakinga na maafa, na tayari ilishadaiwa kuwa toka ujenzi huo uanze tayari mafundi zaidi ya wawili walishaanguka mahali hapo.

Hata hivyo juhudi zakumsaka mkandarasi anayeendesha ujenzi mahali hapo hazikuzaa matunda na hakupatikana kwa kuwa hakujulikana.

source nifahamishe

0 comments:

Post a Comment