Mshindi wa Tuzo Milionea Akabidhiwa Milioni 100 Zake

Sunday, May 16, 2010 / Posted by ishak /


Kampuni ya simu za mkononi ya Vodacom Tanzania imemkabidhi hundi ya shilingi milioni 100 mshindi wa Promosheni ya Tuzo milionea Bw. Bernard John (27) mkazi wa Morogoro.
Bw. Bernard John (27) alikabidhiwa mshiko wake katika hafla fupi iliyofanyika nyumbani kwake na kuhudhuriwa na maofisa wa Vodacom ndugu jamaa na marafiki.

Ujumbe wa Vodacom Tanzania uliongozwa na Mkuu wa Uendeshaji wa Vodacom Tanzania Peter Correia ambaye pamoja na mambo mengine alimpongeza mshindi huyo na kumshauri azitumie fedha hizo kuboresha maisha yake.

“Kwa niaba ya Vodacom Tanzania, ninapenda kuchukua fursa hii kukupongeza sana ni furaha iliyoje kuona mwenzetu katika familia kubwa ya Vodacom Tanzania yenye wateja zaidi ya milioni saba anabadilisha maisha yake kwa kuyaboresha,” alisema.

John alishinda kupitia droo kubwa iliyochezeshwa na kampuni hiyo na kuonyeshwa moja kwa moja kupitia kituo cha televisheni cha ITV chini ya usimamizi wa bodi ya michezo ya kubahatisha nchini.

Akiongea katika hafla hiyo, John aliishukuru Vodacom kwa kuanzisha promosheni hiyo ambayo alisema inaboresha maisha ya wateja wa Vodacom.

“Kwakweli ninaipongeza Vodacom Tanzania kwa kuanzisha promosheni hii ambayo imebadilisha kabisa maisha yangu na kuwa yenye matumaini, nitazitumia fedha hizi kwa kujiendeleza zaidi kielimu na manufaa ya familia yangu na jamii yangu inayonizunguka,”alisema.

Promosheni ya Tuzo Milionea kwa mwaka huu, ilianza mapema mwezi Februari lengo likiwa ni kuwarejeshea wateja wa Vodacom sehemu ya kile Vodacom inachokipata na pia kuboresha maisha ya wateja wake.

Correia alifafanua kuwa tangu kuanza kwa promosheni hiyo ambayo imedumu kwa miezi mitatu sasa, wateja wa wameweza kujishindia zawadi mbalimbali zikiwa ni pamoja na muda wa maongezi.

Correia alisema kuwa kupitia Promosheni ya Tuzo Milionea, wateja Saba wa Vodacom walijishindia muda wa maongezi wenye thamani ya sh. 100,000 kupitia droo za kila wiki na hadi mwisho wa promosheni hiyo wateja wetu watajishindia muda wa maongezi wenye thamani ya shilingi milioni tisa.

Aidha aliongeza kuwa Promosheni hii ni mwendelezo wa promosheni ya Tuzo milionea iliyoendeshwa na Vodacom Tanzania kwa mwaka jana.

“Kama mtakumbuka mshindi wa droo kubwa ya mwaka jana alikuwa ni Renatus Mkinga, Mkazi wa Mombasa, Ukonga Jijini Dar es Salaam, ambaye alishinda shilingi milioni 100 na kuboresha maisha yake”.

Akitoa wito kwa wateja wengine kushiriki mara nyingi katika promosheni mbalimbali zinazochezeshwa na kampuni hiyo kwa siku za usoni Bw Correia aliwahakikishia kuwa zitawawezesha kuibuka kidedea na kuboresha maisha yao.

“Tutaendelea kuwekeza ili kuboresha huduma zetu mbalimbali kwa kuwa tunaamini kwamba huduma bora na za uhakika za mawasiliano ni sehemu ya maendeleo, kwani maendeleo ya nchi yoyote yanachangiwa na huduma za mawasiliano zenye uhakika” Alisema.

source nifahamishe

0 comments:

Post a Comment