Mwanasiasa wa Nigeria Akamatwa na kilo 2 za Cocaine Tumboni

Wednesday, May 19, 2010 / Posted by ishak /


Mwanasiasa wa Nigeria ametiwa mbaroni nchini humo baada ya kunaswa uwanja wa ndege akiwa amemeza kilo mbili za madawa ya kulevya aina ya cocaine.
Polisi nchini Nigeria walisema kuwa mwanasiasa huyo aliyegombea ubunge wakati wa uchaguzi uliopita na ambaye pia anagombea ubunge katika uchaguzi ujao, alikamatwa kwenye uwanja wa ndege wa Lagos akiwa amemeza kilo mbili za madawa ya kulevya aina ya cocaine akijaribu kuzisafirisha kuzipeleka Ujerumani.

Mwanasiasa huyo aliyetajwa jina lake kuwa ni Eme Zuru Ayortor aliwaambia maafisa wa polisi kuwa alimeza madawa hayo ya kulevya ili aweze kupata pesa za kupigia kampeni wakati wa uchaguzi.

Polisi walisema kuwa scanners za uwanja wa ndege zilionyesha kete za madawa ya kulevya zikiwa tumboni mwa mwanasiasa huyo mwenye umri wa miaka 52.

Polisi walisema kuwa walifanikiwa kuzipata kete 100 za cocaine toka kwenye tumbo lake.

Taarifa zilisema kuwa Ayortor aliwaambia polisi kuwa alihitaji pesa kwakuwa alipoteza pesa nyingi sana wakati wa kampeni za uchaguzi uliopita wa mwaka 2007.

"Kiasi cha madawa ya kulevya alichokibeba tumboni ni kikubwa sana", alisema afisa wa polisi na kuongeza "Tunaamini hii sio mara yake ya kwanza kusafirisha madawa ya kulevya".

Kitaaluma Ayortor, ana shahada ya pharmacy aliyoipata kwenye chuo kikuu cha Wisconsin nchini Marekani.

source nifahamishe

0 comments:

Post a Comment