Watu 60 Wafariki Kwasababu ya Mtu Mmoja

Wednesday, May 26, 2010 / Posted by ishak /


Watu 60 wameishafariki nchini Jamaica hadi sasa kufuatia vurugu zilizozuka wakati polisi wa Jamaica walipoanzisha msako wa nyumba kwa nyumba ili kumkamata kiongozi wa kundi la wauzaji wa madawa ya kulevya wa Jamaica ambaye Wamarekani wanataka akamatwe apelekwe nchini Marekani kushtakiwa.
Mamia ya wanajeshi na polisi walivamia magheto ambayo kiongozi wa kundi la wauza madawa ya kulevya wa Jamaica, Christopher Coke au maarufu kama "Dudus" anaaminika kuwa amejificha katika jiji la Kingston.

Vurugu kubwa zilizuka baada ya wananchi wanaomtetea Dudus kuamua kuwashambulia polisi kupinga kukamatwa kwake.

Dudus anatakiwa nchini Marekani kutokana na kujihusisha kwake na biashara za madawa ya kulevya na silaha.

Dudus mwenye umri wa miaka 41 ana wafuasi wengi toka kwenye makazi ya watu maskini wa mjini Kingston ambao wamesema wako tayari kumlinda Dudus kwa gharama yoyote ile.

Dudus ambaye wafuasi wake wanapenda kumwita "rais" hapendi kuvaa nguo za gharama na huwa haonyeshi ufahari anapokuwa kwenye klabu za starehe kama ambavyo mabosi wengine wa makundi ya uuzaji wa madawa ya kulevya hupenda kujionyesha.

Vurugu hizo zimeingia siku ya tatu mfululizo ambapo Dudus hadi sasa hajakamatwa lakini jumla ya watu 60 wameishapoteza maisha yao.

Wafuasi wa Dudus wamekuwa wakirushiana risasi na wanajeshi na polisi kupinga kukamatwa kwake.

Kutokana na vurugu hizo kusambaa maeneo mengi ya mji wa Kingston, shule na biashara nyingi mjini humo zimefungwa.

Mpambano mkubwa wa polisi na wafuasi wa Dudus unaendelea kwenye magheto ya Trenchtown ambako nyota wa muziki wa reggae Bob Marley ndiko alikokulia

source nifahamishe

0 comments:

Post a Comment