Zawadi ya Kiongozi Bora Afrika Yakosa Mshindi

Wednesday, June 16, 2010 / Posted by ishak /


Kwa mwaka wa pili mfululizo mshindi hajapatikana kwaajili ya zawadi ya dola milioni 5 ya kiongozi bora wa Afrika ambaye ameonyesha mfano wa uadilifu katika uongozi na serikali ya kidemokrasia.
Wadhamini wa tuzo ya kiongozi bora wa Afrika wamesema kuwa mwaka huu pia wameshindwa kumpata kiongozi wa nchi aliyeonyesha mfano wa uongozi bora na serikali ya kidemokrasia.

Washindi wa tuzo ya kiongozi bora wa Afrika hupewa zawadi ya dola milioni 5 ndani ya kipindi cha miaka 10 na baada ya miaka 10 kuisha hupewa dola laki mbili kila mwaka kwa miaka yote ya maisha yao iliyobaki.

Mo Ibrahim, mfanyabiashara bilionea aliyezaliwa nchini Sudan ndiye aliyeanzisha tuzo hizo mwaka 2006 ili kuwapa moyo viongozi wa Afrika kuongoza serikali zao kwa misingi bora ya uongozi.

Kamati huru ya watu saba ikiongozwa na katibu mstaafu wa umoja wa mataifa, Kofi Annan, ilikutana tena jumamosi lakini ilishindwa kumchagua mshindi.

Kamati hiyo pia mwaka jana ilishindwa kumchagua kiongozi yoyote wa Afrika kushinda tuzo hiyo.

Tuzo hiyo hutolewa kwa viongozi wa Afrika waliochaguliwa kidemokrasia ambao wameachia madaraka ndani ya miaka mitatu iliyopita.

"Sifa za viongozi bora zilizowekwa ziko juu na kila mwaka idadi ndogo ya viongozi wenye sifa hupatikana. Kwahiyo kuna uwezekano miaka mingine hatapatikana mshindi", alisema Mo Ibrahim.

Hadi sasa ni viongozi wawili tu wa Afrika ambao wamezawadia tuzo hiyo, rais mstaafu wa Botwana, Festus Mogae na rais mstaafu wa Msumbiji, Joaquim Chissano. Rais wa zamani wa Afrika Kusini, Nelson Mandela alipewa tuzo maalumu ya heshima mwaka 2007.

source nifahamishe

0 comments:

Post a Comment