Mwarabu Atupwa Jela Kwa Kufanya Mapenzi na Myahudi

Thursday, July 22, 2010 / Posted by ishak /


Mwanaume mmoja wa kiarabu wa nchini Israel ametupwa jela miezi 18 baada ya kugundulika kuwa alikuwa na uhusiano wa kimapenzi na mwanamke wa kiyahudi baada ya kumuongopea kuwa yeye ni Myahudi.
Mahakama ya wilaya ya Jerusalem imemhukumu Sabbar Kashur mwenye umri wa miaka 30 kwenda jela mwaka mmoja na nusu kwa kosa lililohesabika kama kubaka kwa kufanya mapenzi na mwanamke wa kiyahudi baada ya kumuongopea kuwa yeye ni myahudi anayetaka uhusiano wa kimapenzi wa muda mrefu.

Kashur alifanikiwa kuanza uhusiano wa kimapenzi na mwanamke huyo lakini baada ya mwanamke huyo kugundua kuwa Kashur si myahudi kama alivyodai, alienda polisi kushtaki na Kashur alitiwa mbaroni akikabiliwa na kosa la ubakaji, limeripoti gazeti la Haaretz la Israel.

"Kama angejua kuwa mtuhumiwa si myahudi anayetaka uhusiano wa kimapenzi wa muda mrefu, asingemkubalia", alisema jaji Zvi Segal wakati akitoa hukumu.

Kashur ambaye ameoa na ana watoto wawili wadogo, ameiita hukumu hiyo kuwa ni ya kibaguzi.

"Kama mimi ningekuwa ni myahudi, wala wasingeniuliza kitu, huwezi kusema nimebaka", gazeti la Haaretz lilimnukuu Kashur.

"Alikubali mwenyewe bila kulazimishwa kila kitu ambacho kilitokea".

Kutumia uongo ili kuweza kumlaghai mwanamke na kufanya naye mapenzi huhesabika ni kubaka kwa mujibu wa sheria ambayo iliwekwa mwaka 2008 nchini humo baada ya mwanaume mmoja kujifanya yeye ni afisa wa masuala ya majumba ambaye aliwaahidi kuwapatia nyumba wanawake ambao angefanya nao mapenzi.

Kuna waarabu milioni 1.3 nchini Israel ambao ni sawa na asilimia 20 ya watu wote nchini humo.


source nifahamishe

0 comments:

Post a Comment