Kitabu cha Katuni za Kumkashifu Mtume Kutolewa Mwezi Ujao

Friday, August 27, 2010 / Posted by ishak /


Mwandishi wa habari wa Denmark ambaye alisababisha mtafaruku duniani alipotoa katuni za kumkashifu mtume Muhammad (s.a.w) kwenye gazeti, ametangaza kuwa atatoa kitabu mwezi ujao chenye katuni hizo.
Mwandishi wa habari wa Denmark ambaye mwaka 2005 alichapisha katuni 12 za kumkashifu mtume Muhammad (s.a.w) kwenye gazeti, ametangaza kuwa kitabu kipya chenye katuni hizo kinatoka mwezi ujao.

Kitabu hicho kilichoandikwa na mhariri wa gazeti la Jyllands-Posten, Flemming Rose kitaingia madukani septemba 30 ikiwa ni miaka mitano tangu katuni hizo zilipochapishwa kwenye gazeti.

Kuchapishwa kwa katuni hizo kulisababisha mtafaruku duniani na kupelekea baadhi ya watu kufariki katika maeneo mbalimbali duniani.

Katika mahojiano na gazeti la Denmark la Politiken, Rose alisema kuwa hataki kuleta chokochoko lakini anataka watu wazifahamu katuni 12 pamoja na picha zingine ambazo zinadaiwa kuwa ni za uchochezi.

"Najua watu wengi hawaelewi nafikiria nini kuhusiana na katuni hizi, nataka nijielezee mwenyewe, sina chochote zaidi ya kutumia maneno kuelezea .. baada ya watu kukisoma kitabu nadhani wataelewa ukweli wa mambo. Maneno yajibiwe kwa maneno, hivyo ndivyo inavyotakiwa kwenye demokrasia", alisema Rose.

Rose ambaye alitumiwa vitisho vingi vya kuuliwa alipochapisha kwa mara ya kwanza katuni hizo, alisema kuwa anataka kuanzisha mjadala barani ulaya kuhusiana na jinsi watu wanavyotakiwa kuishi kwenye karne ya 21. "Mgogoro wa katuni umeonyesha tutegemee nini kwenye karne ya 21", alisema.

Naye msanii wa katuni wa Denmark, Kurt Westergaard, ambaye alichora katuni ya mtume iliyomuingiza matatani kwa kuchora katuni aliyodai ya mtume ikiwa na bomu kwenye kilemba, naye ametangaza kuchapisha kitabu cha katuni zake hizo ndani ya miezi michache ijayo.

Mwanzoni mwa mwezi huu gazeti la Jyllands-Posten lililochapisha katuni hizo lilitangaza kuwa limeweka fensi za umeme kwenye ofisi zake ili kujilinda na mashambulizi ya kigaidi.

source nifahamishe

0 comments:

Post a Comment