Mama Asiyetaka Watoto Aua Watoto Wake 8 na Kuwafukia

Sunday, August 01, 2010 / Posted by ishak /


Mwanamke mmoja wa nchini Ufaransa ambaye baada ya kujifungua watoto wawili alikuwa hataki tena kupata watoto wengine, hakutaka kutumia kinga wakati wa kujamiiana na alipopata ujauzito aliwaua watoto wake wanane aliowazaa bila ya mumewe kujua.
Mwanamama Dominique Cottrez mwenye umri wa miaka 47 wa mji wa Lille nchini Ufaransa amekuwa gumzo nchini humo baada ya kukiri kuwaua watoto wake wanane aliowazaa bila ya mumewe kugundua.

Dominique anashikiliwa na polisi huku uchunguzi ukiendelea wakati mumewe ameachiwa huru.

Dominique aliwaambia polisi kuwa hakutaka kupata watoto wengine baada ya kuzaa watoto wawili kwa tabu kutokana na unene aliokuwa nao lakini pia hakutaka kutumia kinga wala kuomba ushauri wa madaktari kujizuia kupata ujauzito tena.

Dominique alisema kuwa alipopata ujauzito alikuwa akifanya siri bila ya mumewe kujua na alipojifungua aliviua vichanga vyake na kuvifunga kwenye plastiki kabla ya kuvifukia chini ya ardhi.

Dominique aliwaambia wapelelezi kuwa wakati wa ujauzito alitumia muda mwingi peke yake na alikuwa akijizalisha mwenyewe bila ya msaada wa mtu yoyote.

Vichanga vinane alivyoviua vilizaliwa kati ya mwaka 1987 na 2007.

Ukatili wa Dominique uligundulika baada ya wapangaji kuhamia kwenye nyumba aliyokuwa akiishi awali ambapo maiti za vichanga viwili ziligunduliwa chini ya ardhi kwenye bustani ya nyumba hiyo.

Maiti zingine sita ziligunduliwa kwenye gereji ya nyumba aliyokuwa akiishi na mumewe.

Taarifa zinasema kuwa Dominique na mumewe ni watu waliokuwa wakijulikana na kuheshimika sana kwenye kijiji chao cha Villers-au-Tertre.

Dominique alikuwa akifanya kazi kama nesi wakati mumewe alikuwa akifanya kazi za ujenzi.

Wanakiji na watu wanaomjua Dominique na mumewe wameelezea kupigwa na butwaa na habari hizi kwakuwa Dominique na mumewe walikuwa ni watu wanaopenda kusaidia watu na kujishughulisha katika shughuli mbalimbali za jamii.

Watoto wawili wa mwanzo wa Dominique ambao hivi sasa wana umri wa miaka 21 na 22, nao wameelezea kusikitishwa na habari hizi wakisema kuwa hawajui ni nini kilichomsibu mama yao mpaka akaamua kufanya ukatili huo.

source nifahamishe

0 comments:

Post a Comment