Mamba Aiangusha Ndege Kongo, 20 Wafariki

Sunday, October 24, 2010 / Posted by ishak /


Watu 20 wamepoteza maisha yao nchini Kongo baada ya ndege waliyokuwamo kuanguka toka angani baada ya mamba aliyeingizwa kinyemela ndani ya ndege hiyo kuchoropoka na kuleta kizazaa kikubwa ndani ya ndege.
Abiria aliyetaka kumsafirisha mamba wake kinyemela kwa kumficha mamba huyo ndani ya begi na kuingia nalo ndani ya ndege amesababisha vifo vya watu 20.

Ni mtu mmoja tu kati ya watu 21 waliokuwemo ndani ya ndege huyo ndiye aliyenusurika maisha yake.

Kwa mujibu wa abiria huyo aliyeponea chupu chupu kupoteza maisha yake, mamba huyo aliyekuwa amefichwa ndani ya begi na kuingizwa kinyemela ndani ya ndege nchini Kongo alisababisha mtafaruku mkubwa ndani ya ndege na kupelekea ndege kuanguka.

Mamba huyo alichoropoka toka kwenye begi wakati ndege ndogo ya abiria iliyotengenezwa nchini Czech aina ya Let 410 ilipokuwa angani ikitoka mji wa Kinshasa kuelekea Bandundu.

Ilikuwa ni patashika nguo kuchanika wakati mamba huyo alipoanza kuranda randa ndani ya ndege na kupelekea abiria waviache viti vyao kusalimisha maisha yao.

Wahudumu wa ndani ya ndege walikimbilia ndani ya chumba cha marubani na kufuatiwa na baadhi ya abiria ambao nao waliamua kuitumia nafasi hiyo kusalimisha maisha yao.

Inasemekana kuwa ndege hiyo ilianguka toka angani kutokana na uzito ndani ya ndege kuelemea upande mmoja.

Ndege hiyo iliangukia kwenye nyumba iliyopo maili chache toka kwenye uwanja wa ndege ambao ndege hiyo ilipanga kutua.

Mamba aliyesababisha ajali hiyo alitoka salama salimini toka kwenye mabaki ya ndege hiyo lakini aliuliwa kwa kuchomwachomwa na kisu na watu waliojitokeza kuwaokoa majeruhi wa ajali hiyo.

source nifahamishe

0 comments:

Post a Comment