Kidedea: Kikundi cha sanaa kilichoweka mapenzi pembeni na kufanya kazi

Saturday, February 13, 2010 / Posted by ishak / comments (0)


KWA wapenzi wa sanaa ya maigizo bila shaka wanaweza kuyakumbuka majina kama Peace ambaye kwa sasa ni marehemu, Jengua na mengine kadhaa yaliyokuwa yakiunda kikundi maarufu cha Kidedea, kikundi hicho kimerudi tena upya kikiwa na wasanii zaidi ya 50.
Kikundi hicho kilipata umaarufu wake kupitia michezo ya kuigiza kwenye televisheni kiasi cha wasanii wa kikundi hicho kupata kero kubwa wanapofanya shuguli zao za kawaida mitaani au wanapokuwa katika matembezi ya kawaida.

Hata hivyo umaarufu wa kikundi hicho ulizimika ghafla katikati ya miaka ya 2000 baada ya wasanii wa kikundi hicho kusambaratika na kuunda vikundi vingine vidogo vilivyokosa msisimko.

Hatimaye hii leo tunakizungumzia kikundi hicho kikiwa hai, kufuatia juhudi kubwa za mlezi na mdhamini wake wa sasa Dk Karim Kihiyo ambaye pia ni Mkurugenzi wa kituo cha tiba asilia zilizotafitiwa kisasa cha The Modern Traditonal Clinic.

Kwa sasa kikundi hicho kimepiga maskani yake katika ukumbi wa CCM Manzese Tip Top kikifanya mazoezi makali huku kikiwa na wasanii wasiopungua 58 wanaofanya maonyesho yote yanayohusu sanaa.

Tofauti na ilivyokuwa zamani ambapo kikundi hicho kiliegemea sana katika sanaa za maonyesho kwa kufanya kazi kwenye vituo vya televisheni pekee, hivi sasa sanaa katika kikundi hicho kimegawanyika katika sehemu kuu tatu.

Kwa mujibu wa Mkurugenzi huyo ndani ya Kikundi hicho cha Kidedea sasa kuna kitengo cha muziki wa asili ambapo ngoma za makabila mbalimbali ya ndani na nje ya nchi hutumbuizwa kwa umahiri mkubwa.

Vilevile muziki wa dansi kutoka karibuni pande zote za dunia likiwemo Bara Hindi hutumbuizwa kwa kupigwa 'Live' na hata kuchezwa na wasanii wa kikundi hico wanaoonekana kuiva haswa katika fani ya sanaa.

Kwa leo hii utakapopata bahati ya kuingia katika ukumbi wa CCM Manzese Tip Top na ukiwakuta wasanii wakiwa mazoezini utaamini kwamba hivi sasa wamedhamiria kuingia kwenye sanaa kwa nguvu zote.

"Kidedea" ni neno linalotamkwa na kiongozi wa kikundi hicho ambapo baadae wasanii hujibu kwa pamoja na kwa sauti kuu maneno haya.

"Kanyage twende, tunapendana bila kutakana, hapa ni kazi tu mapenzi kwenu'

Maneno haya hayatamkwi kwa mzaha, bali wasanii wanapoapa kipo hiki huonyesha dhamira kutoka mioyoni mwao huku baadhi yao wakionyesha ishara ya kugangamaa kwa kutumia miguu, mikono na hata vichwa ili kukipa nguvu kiapo chao.

Dk Karim Kihiyo katika mahojiano na Nifahamishe alisema kwamba muundo wa sasa wa kikundi cha Kidedea umelenga biashara zaidi na kumnufaisha msanii mmoja baada ya mwingine tofauti na ilivyokuwa zamani ambapo faida ya msanii ilikuwa ni kuonekana kwenye luninga.

Anasema katika kuhakikisha kuwa wasanii wananufaika na kundi lao wanatumia fani mbalimbali ikiwa ni kwa kushiriki katika shughuli mbalimbali ambazo zinafanyika katika jamii.

Kihiyo anasema kwa sasa wanajipanga vilivyo ili kuhakikisha kuwa kila kundi ambalo linaunda kidedea linasimama imara kwa kuhakikisha kuwa linatoa mchango wake kwa kila hali na mali.

Mkurugenzi huyo wa Kidedea anasema kuwa kwa sasa wanatarajia kutumia maonyesho mbalimbali pamoja na mabonanza ambayo yatakuwa yakifanyika sehemu za wazi kujitangaza kwa wapenzi wao.

Anasema kuwa pamoja na wao kushiriki katika mabonanza pia wataanza ya kwao wenyewe katika siku za mwisho wa wiki ambapo wanatarajia kutoa burudani ya kila aina.

"Na katika kuhakikishia kuwa tumerudi kwa kasi kubwa na matunda yetu yataanza kuoekana siku karibuni kwani kwa sasa tunajinoa vya kutosha," alisema.

Kihiyo aliweka bayana kuwa kikundi chake kimejipanga kukabiliana na changamoto mbalimbali ambazo zitajitokeza kwani hizo ndizo zilichangia kuyumba katika kipindi kilichopita.

Aliweka bayana kuwa mikakati yao ni kuhakikisha kuwa burudani ya asili inarudi kama ilivyokuwa hapo awali.

Anasema kuwa kundi hilo lenye wasanii 58 limezingatia vigezo mbalimbali katika kuwapata ambapo asilimia kubwa ya washiriki ni vijana.

Mkurugenzi huyo anasema pamoja na kuzingatia suala la umri pia wamejitahidi kuepuka watu ambao wanajiona kuwa ni maarufu kwani walio wengi wamekuwa wakichangia migogoro ndani ya makundi kama hayo.

"Katika kundi letu hakuna mtu ambaye atajiona yeye ni maarufu (star) wote ni sawa na hilo tutalisimamia kwani kinachohitajika hapa ni kazi mbele na mambo mengine hayana nafasi," alisema.

Alisema pamoja na kazi pia tunadumisha ushirikiano baina yetu kwani hiyo ni moja ya nguzo muhimu kwa sisi kufikia malengo ambayo tumejiwekea ambayo ni ya kila msanii kufaidika na kundi.

Alisema katika kundi hilo yupo msanii maarufu kama Mzee Kankaa lakini ameahidi kutumia uwezo wake kusaidia mafaniko ya kundi na washiriki wote kwa ujumla.

Dk. Kihiyo amewataka wadau na wapenzi wa kundi la kidedea kuunga mkono kundi hilo ambalo limedhamiria kutoa burudani ya kutosha kwa kipindi hiki na kijacho.

source nifahamishe

Sinema ya Kutisha Yasababisha Watu Wakimbizwe Hospitali

Saturday, February 13, 2010 / Posted by ishak / comments (0)


Sinema ya kutisha ya 'Paranormal Activity' imezua kasheshe nchini Italia baada ya msichana mmoja kupooza mwili wake na watu wengi walioiangalia filamu hiyo kuwahishwa hospitali wakiwa hawajitambui.
Filamu hiyo iliingia kwenye kumbi za sinema za Italia bila kuwekwa katika fungu lolote la umri tofauti na Marekani ambako iliwekwa katika fungu la watu wazima "R" na nchini Uingereza ambako watu wenye umri chini ya miaka 15 hawakutakiwa kuiangalia filamu hiyo.

Hivi sasa kuna shinikizo kubwa nchini Italia wazazi wakitaka filamu hiyo ionyweshwe kwa watu wenye umri zaidi ya miaka 18 pekee.

Kwa jinsi filamu hiyo ilivyofanikiwa kuwatisha watu wengi, huduma za dharura za hospitali nchini Italia ziliwapokea mamia ya watu walioiangalia filamu hiyo siku ya jumamosi ambao walishindwa kujitambua kutokana na kupaniki.

Hata tangazo la filamu hiyo linadaiwa kuwatisha maelfu ya watoto lilipoonyeshwa kwenye televisheni za Italia.

Hali ilikuwa mbaya zaidi kwa msichana mmoja mwenye umri wa miaka 14 ambaye aliwahishwa hospitali akiwa amepooza mwili wake baada ya kuangalia filamu hiyo.

Hata waziri wa ulinzi wa Italia, Ignazio La Russa, ameingia kwenye zogo la filamu hiyo akisema kuwa kwa wiki mbili tangazo la filamu hiyo limekuwa likiwatisha sana watoto linapoonyeshwa mara kwa mara kwenye televisheni za Italia.

"Inatisha kweli, nakumbuka wakati mtoto wangu wa kiume wa miaka saba aliponiambia "Baba Naogopa" alipoona tangazo la filamu hii", alisema waziri huyo wa ulinzi.

Filamu ya Paranormal Activity ilitengenezwa kienyeji kwenye nyumba ya
mtayarishaji wake Mmarekani Oren Peli. Sinema hiyo iligharimu dola 15,000 tu tofauti na filamu za Hollywood ambazo hugharimu mamilioni ya dola.

Hata hivyo ilipoingia kwenye kumbi za sinema nchini Marekani mwezi oktoba mwaka jana ilifanikiwa kuingiza dola milioni 22 ndani ya wiki moja.

source nifahamishe

Nyota wa Muziki wa Pop wa Ujerumani Awaambukiza Ukimwi Wanaume Watatu

Saturday, February 13, 2010 / Posted by ishak / comments (0)


Mahakama ya nchini Ujerumani imemuona nyota maarufu wa muziki wa Pop, Nadja Benaissa wa kundi la waimbaji wanawake la 'No Angels' ana hatia ya kuwaambukiza ukimwi wanaume watatu aliofanya nao mapenzi bila kinga huku akijijua kuwa yeye ni muathirika.
Waendesha mashtaka wa Ujerumani jana ijumaa walimuona msanii maarufu wa kundi la "No Angles" Nadja Benaissa mwenye umri wa miaka 27 ana hatia ya kuwaambukiza ukimwi wanaume watatu aliofanya nao mapenzi bila kinga.

Nadja anadaiwa kufanya mapenzi na wanaume hao kati ya mwaka 2000 na 2004 bila kuwataarifu kuwa yeye ni muathirika.

Nadja alikuwa akijitambua fika kuwa yeye ni muathirika tangia mwaka 1999, nyaraka za mahakama zilisema.

"Alikuwa akijua wazi kuwa kwa kufanya mapenzi bila kinga atawaambukiza maradhi yake wanaume hao", alisema mwendesha mashtaka katika mji wa Darmstadt ulio jirani na Frankfurt.

Mmoja wa wanaume hao watatu ameishathibitishwa kuwa ameambukizwa virusi vya HIV vinavyosababisha ukimwi.

Kundi la No Angeles liliibuliwa na mashindano ya vipaji kwenye luninga mwaka 2000 na baada ya kujipatia umaarufu mkubwa walifanya ziara nyingi sana barani ulaya kabla ya kundi hilo kuvunjika mwaka 2003.


source nifahamishe

Atoweka nyumbani baada ya kupata ‘0’ matokeo ya kidato cha nne

Friday, February 12, 2010 / Posted by ishak / comments (0)

MSICHANA Joyce Aloyce [18] mkazi wa Shekilango jijini Dar es Salam, ametoweka nyumbani kwao baada ya kupata majibu yake ya kidato cha nne yaliyoonyehsa amefeli mitihani hiyo na kupata divisheni 0.

Msichana huyo ametoweka nyumbani kwao na hajulikani alipo na mama yake kupata na wasiwasi na kujua mwanae huyo yuko wapi na hajui pa kumpata wapi.

Mama huyo aliyekutana na Mwandishi wa habari hii katika kutuo cha Urafiki cha jijini akija kuripoti tukio hilo kwa msaada zaidi.

Mama huyo aliiambia nifahamishe kuwa binti yake huyo hamuoni takribani wiki sasa na kusema toka matokeo hao yatoke na kujigundua kuwa alipata ziro basi hakurudi nyumbani hapo kwa kuhofia kufukuzwa nyumbani kwao hapo kwa kuwa mzazi ake wa kumu alishamwambia awali kabla ya matokeo.

Alidai walipoona kinywa kinazidi walijaribu kupita kwa ndugu zao wa karibu ambao wangehisi labda angekuwa huko lakini bila mafanikio hawakuweza kumkuta wka ndugu yoyote na kutojua yuko wapi kwa sasa.

Alidai kutokana na hali hiyo familia hiyo wameanza kuogopa na wamekuja kuripoti kituoni hapo na taratibu zingine zinaendela za kwenda kumsaka na mikoni huenda atakuwa amekwena kujichimbia huko kwa kujhofia aibu na kupigwa na baba yake.

Mama huyo alidai binti huyo ni mtoto wake wa pili na kuonyesha huzni kubwa kwa kuwa motto wa kike katika familia hiyo hiyo aliuwa jni yeye tu kati ya watoto wannne alio nao.

“Mimi naweza kumsamehe hata akirudi nyumbani ila mume wangu sijui kama ataweza kumsamehe, wanaume wanakuwa wakali hata watoto wanawaogopa sasa mwanangu ametoweka nyumbani kwa kumuogopa baba yake” huku akionekana kutokwa na machozi kwa mkasa huo uliomkuta


source nifahamishe

Nguza, Papii Kocha ndo basi tena uraiani

Friday, February 12, 2010 / Posted by ishak / comments (0)



VILIO simanzi vilitawala jana katika viwanja vya Mahakama ya Rufani baada ya Jaji Neema Chusi kutangaza kuwaachia huru watoto wawili wa Nguza Viking kwa kile alichosema walifungwa kimakosa na hawakuhusika katika kesi ya msingi .


Hukumu hiyo iliyoanzwa kusomwa saa 3 za asubuhi jana, ambapo umati mkubwa wa watu kutoka kona mbalimbali za jijini Dar es Salaam na wanamuziki mbalimbali nchini walifurika kushuhudia hatma ya rufaa ya wanamuziki hao waliyowsilisha katika mahakama hiyo.


Katika mashitaka ya kubaka Jaji Chusi alisema kuwa, jopo lililokuwa likisikiliza rufani hiyo limebaini kuwa, katika mashitaka 10 ya kubaka yaliyokuwa yakiwakabili wafungwa hao Francis Nguza na mdogo wake Mbangu Nguza hawakuhusika nalo kabisa.

Alisema kuwa ushahidi unaonesha wazi kuwa wakati makosa hayo yakitendeka mtoto mmoja alikuwa shuleni na mwenzake alikuwa ziarani mikoani.

Na kusema kuwa upande wa mashitaka uliowasilishwa katika Mahakama ya Kisutu haikufuata sheria juu ya ushahidi uliotolewa kama kosa la kubaka lililokuwepo mahakamani kwakuwa haikuwepo PF 3 toka Hospitali ya Mwananyamala kwa maelezo.

Aliongeza kuwa japo ushahidi wa mshitakiwa una mapungufu lakini ushahidi uliotolewa na Dk.Pretoria Ngeloi alidai kuwa, baadhi ya watoto waliobakwa na wanamuziki hao walikutwa na maambukizi ya ugonjwa wa gono.

Alisema kuwa ushahidi uliotolewa kwa pande zote mbili ziliridhika na washitakiwa walihusika kwa makosa ya kubaka na kulawiti.

Hivyo majaji waliona kuwa katika mashitaka hayo Babu Seya na Papii Kocha waliyatenda wote kwa pamoja na watoto hao wawili hawakuhusika katika ubakaji huo.

Akitoa hukumu hiyo Chusi alisema kuwa washitakiwa hao walipatikana na mashitaka 5 ambapo mashitaka 11 ya kulawiti alisema kuwa, walibaini kuwa wafungwa hao wote hawakuyatenda bali yalitungwa kwa nia ya kuwakandamiza zaidi.

Kutokana na kauli hiyo Babu Seya na wanawe walianza kuangua vilio na familia ya mwanamuziki huyo hali iliyosababisha ndugu, jamaa na watu waliofurika mahakamani hapo kuanza kuangua vilio kwa kauliu hiyo ya Jaji Chusi.

Hivyo wafungwa hao ambao walishaanza nklutumiki kifungo hicho jana waligonga mwamba dhidi ya rufani yao na wameruishwa kwenda kutumikia kifungo hicho tena.

Baadhi ya watu waliweza kuhojiwa na NIFAHAMISHe alisem kwu wanaiomba serikali kuweza kuangalia zaidi sakata hilo kwani hata kuachiwa kwa watoto hao ni huzuni kwa kuwa mzazi wao ambao ni tegemeo lao amerudishwa gerezani.

Kwa upande wa mawakili wanaowatetea wafungwa hao waliiomba mahakama iwachie huru wanamuziki hao kwa kuwa hukumu iliyowatia hatiani ilikuwa na dosari nyingi za kisheria.

Pia walidai kuwa kesi hiyo ilikuwa ya kupangwa na kwamba hawajawahi kuona hukumu ya hovyo ya aina hiyo tangu waanze kufanyakazi ya uwakili kwa zaidi ya miaka 30 sasa.

Katika kesi ya msingi wasanii hao walikuwa wakituhumiwa kutenda makosa kumi ya kubaka watoto wenye umri kati ya miaka sita na minane na makosa mengine 11 ya kulawiti watoto wa kike wenye umri huo huo kati ya Aprili na Oktoba mwaka 2003 maeneo ya Sinza jijini Dar es Salaam.

source nifahamishe

Mkapa ni Sawa na Ungo Kwa Majirani, Kibeku Kwa Watanzania

Thursday, February 11, 2010 / Posted by ishak / comments (0)


SIAMINI kama huyu anayezungumziwa hapa ni Rais wangu wa awamu ya tatu nchini Tanzania Benjamin William Mkapa.
Wakati huo nilikuwa najiandaa kuvuka mpaka wa Zambia na Tanzania katika mji wenye vurugu wa Tunduma mkoani Mbeya ili niweze kuingia nchi jirani ya Zambia.

Mbele yangu naona mchanganyiko wa raia wa Tanzania na Zambia wakihangaika huku na huko kujitafutia riziki, wengi wao wakiwa wafanyakazi wa magari ya mizigo.

Mji huu una pilikapilika kama zile za Manzese Jijini Dar es Salaam, lakini hauna tishio la vibaka zaidi ya watu kujitafutia maisha kutokana na shughuli wanazozifanya.

Si rahisi kupata mtu wa kuzungumza naye labda wafanyabiashara wa vyakula waliojitenga kandoni mwa kituo kikuu cha magari yatokayo kila upande.

Uzuri wa sehemu hii ya biashara hakuna anayeilaumu Serikali, wengi wanalaumiana wenyewe kwa wenyewe kwa kuzembea jambo fulani lililowakosesha kipato.

Ukivuka salama kutoka Tunduma utakaribishwa na kitongoji cha Nakonde hapa tayari utakuwa umekanyaga ardhi ya Zambia.

Hapa hakuna pilika pilika nyingi kama zile zilizokuwa Tunduma, watu wanaonekana wakihangaika na shuguli za kawaida, hata wakulima wanaweza kuonekana hapa.

"Murishani anwe" unaweza kuulizwa ikiwa ni salamu ya moja ya kabila moja la nchini Zambia.

Utakapojibu vizuri na kuulizwa nchi uliyotokea na kwa bahati nzuri ukiitaja nchi ya Tanzania hasa Jiji la Dar es Salaam utaongeza heshima kidogo.

Wataanza kudadisi kuhusu masuala ya kisiasa, kiuchumi na mengine kadhaa kuhusu Tanzania.

Humuulizia zaidi Benjamin Mkapa ambaye alipata kuwa Rais wa awamu ya tatu wa Tanzania.

"Murishani Mwapungule Mkapa?" wakiwa na maana anaendeleaje Mheshimiwa Mkapa"

Utakapojibu kwamba hajambo na sasa amejipumzisha ila bado amekuwa akishiriki na ujenzi wa taifa la Tanzania, hawatasita kumpa sifa zake alizojipatia kutokana na uongozi wake shupavu na hapo utaweza kusikia jibu hili.

Wanasema kwamba Mkapa ndiye Rais shupavu wa Tanzania ambaye anapaswa kuwekwa kwenye kumbukumbu za utendaji uliotukuka.

Wanakubali kwamba Tanzania ni moja ya nchi iliyobarikiwa na Mungu kupata viongozi bora tangu aliyekuwa muasisi wa taifa la Tanzania hayati Baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere hadi Rais Kikwete ila kwa Rais mstaafu Mkapa wanazidisha sifa.

Wanamsifu Mkapa kwa namna ambayo hata raia wa Tanzania asingeweza kujua au kueleza sifa ambazo kiongozi huyo anazo.

Ukiachilia kitongoji hicho cha Nakonde utaweza kuvipitia vingine kama vile Mwenzo, Kapwila, Chozi, Chandananeyaya, na Lusiwasi, mji ambao ni makao makuu ya Jimbo la Kaskazini.

Katika vitongoji vya Mfumu, Mpika, Nkulushi River na Chambeshi wanatamani kumuona mkuu huyo wa nchi wa zamani wa Tanzania angalau aende akawatembelee.

Ukitokea Zambia unaweza ukashangazwa na kauli zinazoshabihiana katika miji mbalimbali nchini humo kuhusu sifa za Rais mstafu Mkapa, zinazotokana na uongozi shupavu uliojikita katika kukusanya kodi na kuimarisha miundombinu hasa ile ya barabara.

Wakati unapovuka mpaka wa Tanzania na Malawi ukiwa mjini Kaporo na kuelekea Kalonga maswali ya kuhusu Tanzania na uongozi wake yatazidi kuwa kero kwako.

Unaweza ukatamani usijitambulishe kuwa wewe ni Mtanzania hasa kama hutokuwa na elimu ya kutosha juu ya uraia na hatma ya nchi pamoja na mambo mbalimbali yanayoendelea nchini.

Watakapomtaja Rais Mkapa wataongeza maneno haya nanukuu: 'Sieni Mkapa akale pa pepo'

Maana yake 'mwacheni Mkapa apumzike'.

Wanalaani sana pale wanaposikia kiongozi huyo wa nchi akihusishwa na ubadhirifu.

Ukiweza kukaa katika baadhi ya hoteli zilizopo kwenye miji mikuu kama vile Blantyre au Lilongwe utapata sababu kuu za wananchi hao kumlilia Mkapa.

Kama ilivyo kwa Wazambia huorodhesha kero alizopambana nazo Mkapa katika utawala wake wa awamu ya tatu ya uongozi wa Tanzania.

"Kwanza alipata changamoto ya kwanza kabla ya kugombea Urais kwa vile hakuwa akifahamika sawa kwa Watanzania," anasema mkufunzi wa chuo cha Ualimu Usisya.

"Lakini pia alizuia mfumuko wa bei hadi anaondoka madarakani tulikuwa tumewazidi kwa bei ya vyakula kama vile mchele, unga na hata mafuta huyu aliwawezesha watu wenye kipato cha chini kufurahia maisha," anasema Mwalimu huyo.

Lakini Rais Mkapa anasifiwa kwamba licha ya kumudu kudhibiti mfumuko wa bei lakini ndiye aliyewawezesha Watanzania kupata elimu kuhusiana na uanzishaji wa Mpango wa Maendeleo ya Elimu ya Msingi (MMEM) na Mpango wa Maendeleo wa Elimu ya Sekondari (MMES).

"Mpango huu umeifanya Tanzania itukimbilie kwa kiwango cha elimu, hapo zamani tuliwazidi kabisa," anaongea msomi Alex Chingalaba kutoka mji wa Lumph.

Uthamani wa Rais mstafau Mkapa kwa wananchi wa nchi jirani ni sawa na ungo ingawa hapa nchini thamani yake kwa baadhi ya watu ni sawa na uongo uliochakaa ambao katika baadhi ya maeneo hapa nchini hujulikana kama Kibeku.

Na pindi utakapoaga kutoka kwenye vijiwe hivyo wananchi hao wan chi jirani watakusisitiza kwamba "Nyie Wabongo...Sieni Mkapa".

source nifahamishe

Mwanaume Aliyetuhumiwa Uchawi Auliwa Kwa Mabomu

Thursday, February 11, 2010 / Posted by ishak / comments (0)


Mwanaume mmoja wa nchini Burundi aliyekuwa akituhumiwa kuwaroga ndugu zake, amefariki dunia pamoja na familia yake baada ya bomu kurushwa ndani ya nyumba yake.
Mwanaume huyo alifariki dunia pamoja na watoto wake watatu wakati bomu liliporushwa na kulipuka ndani ya nyumba yake.

Tukio hilo lilitokea jioni ya siku ya jumanne katika kijiji cha Itaba kilichopo ukanda wa kati wa Burundi.

Mwanaume huyo aliyejulikana kwa jina la Emmanuel Nyandwi aliuliwa baada ya kutuhumiwa kumroga mmoja wa ndugu zake na kupelekea kifo chake.

Bomu hilo lilirushwa jikoni kwake wakati Nywandwi alipokuwa amekusanyika na mkewe na watoto wake watatu wenye umri kati ya miaka 7 na 15.

Mabomu yanapatikana kirahisi nchini Burundi na hununuliwa kwa Tsh. elfu moja tu na hutumika zaidi kwenye kutatua migogoro ya ardhi.

Mwaka 2008 pekee watu 130 walifariki dunia baada ya kulipukiwa na mabomu.

source nifahamishe