SIRI ZA MTANDAO WA WIKILEAKS: aliyemhoji Dk Hoseah ni jasusi aliyebobea

Wednesday, December 22, 2010 / Posted by ishak / comments (0)

WAKATI wananchi wakimkosoa mkurugenzi wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru), Dk Edward Hoseah kupinga taarifa ya Wikileaks iliyovujisha mazungumzo yake na ofisa wa ubalozi wa Marekani, imebainika kuwa Mmarekani huyo amepikwa "kijasusi" katika masuala ya usalama wa taifa, uhusiano wa kimataifa, jeshi na ni ofisa mwandamizi.

Ofisa huyo, D. Purnell Delly alipeleka taarifa ya mazungumzo nchini Marekani akiripoti kuwa DK Hoseah amemwambia kuwa Rais Jakaya Kikwete hayuko tayari kuachia sheria ichukue mkondo wake katika kuwashtaki vigogo wanaojihusisha na rushwa.

Dk Hoseah, ambaye kwenye taarifa hiyo anadai kutishiwa maisha kiasi cha kufikiria kuikimbia nchi, amekiri kuongea na ofisa huyo lakini akadai kuwa ofisa huyo alimkariri tofauti na alivyosema.

Katika taarifa yake kwa vyombo vya habari, Dk Hoseah amefafanua kuwa alichokisema ni kwamba Rais Kikwete hayuko tayari kuidhinisha vigogo wanaojihusisha na rushwa kufikishwa mahakamani bila ya kuwa na ushahidi wa kutosha dhidi yao.

Ubalozi wa Marekani umekataa kuzungumzia taarifa hizo za mawasiliano zilizovujishwa na mtandao wa Wikileaks ukisema kuwa hauna maelezo yoyote, kwa mujibu wa mkurugenzi wa kitengo cha mahusiano ya jamii cha ubalozi huo, Ilya D. Levin.

Ikulu ya Dar es salaam nayo haikutaka kuzungumzia suala hilo baada ya Mwananchi kuwasiliana na mwandishi wake, Premmy Kibanga.

Lakini Mwananchi imebaini kuwa ofisa huyo ni mzoefu katika kazi na amepitia mafunzo mbalimbali kiasi cha kumfanya aaminiwe na taifa hilo kubwa kufanya kazi hiyo inayofanana na ya kijasusi kwenye nchi tofauti, baadhi zikiwa ni zile zenye matatizo ya amani.

Taarifa ya Delly kwenda Ikulu ya Marekani ilivujishwa na mtandao wa wikileaks ambao umepata umaarufu mkubwa kwa kutoa siri za serikali mbalimbali duniani.

D. Delly alikuwa mkuu wa ujumbe wa wanadiplomasia wa Marekani kwenye Ofisi za ubalozi jijini Dar es Salaam kuanzia Julai 9, mwaka 2005.

Kabla ya kuja Dar es Salaam kufanya kazi hiyo ya diplomasia, alikuwa msaidizi maalumu wa katibu msaidizi wa masuala ya Afrika kwenye Idara ya Serikali ya Marekani jijini Washington. Alipata nafasi hiyo baada ya kutumikia cheo cha naibu mkuu wa ujumbe wa Marekani jijini Khartoum, Sudan.

Delly alijiunga na idara hiyo mwaka 1983. Awali alikuwa mshauri wa mambo ya siasa na uchumi wa Copenhagen; naibu mshauri wa masuala ya Uchumi jijini Ankara, Uturuki na ofisa katika dawati maalumu nchini Sri Lanka.

Pia alifanya kazi hizo katika miji ya Edinburgh na El Salvador wakati wa vita na akajizolea heshima kubwa na hivyo kutunukiwa tuzo ya ujasiri na utumishi uliotukuka.

Dk Hoseah alieleza kuwa alikaririwa vibaya na ofisa huyo, lakini taarifa zinaonyesha kuwa Delly, ambaye anatokea Jimbo la Virginia, ni mtaalamu wa lugha akiwa amepata shahada yake ya kwanza katika Fasihi ya Lugha ya Kirusi kwenye Chuo Kikuu cha Dartmouth na shahada ya uzamili ya fasihi katika Chuo Kikuu cha Chicago.

Pia Mmarekani huyo alisomea Sheria za Kimataifa kwenye Chuo cha William na Mary, na shahada ya Uzamili ya Usalama wa Kimataifa na Uandaaji wa Mikakati ya Kijeshi katika chuo cha Newport, Rhode Island ambako wanafundishwa askari wa majini.

Chuo cha US Naval alichosomea Delly, ambaye alikuwa mwanachama na mwalimu wa vikosi vya ulinzi vya mwambao wa Marekani, kina kazi ya kuzalisha viongozi wa kuandaa Mikakati ya kijeshi na namna ya kuitekeleza.

Chuo hicho hutoa programu za fani za kijeshi zinazokwenda na wakati, usahihi, mahususi na zinazotekelezeka kwa idadi kubwa ya maofisa wa kijeshi wa Marekani, askari waajiriwa wa majini, waajiriwa raia ndani ya serikali ya Marekani na hata katika taasisi zisizo za kiserikali (NGOs), pamoja na maofisa wa kimataifa.

Chuo hicho hutarajia kupata kundi la viongozi wenye sifa ya uaminifu na kujiamini katika kila jukumu lao na wenye akili za kiutendaji na kimkakati, wenye tafakuri tunduwizi, uwezo mkubwa katika kuunganisha mambo na wapiganaji katika vita.

Mtaala wa chuo umegawika katika kozi kuu tatu za masomo; mikakati na sera, usalama wa taifa katika kufanya maamuzi na namna ya kuunganisha operesheni za kijeshi.

Kozi ya Mikakati na Sera imewekwa kwa ajili ya kuwafundisha wanafunzi kufikiria kulingana na mikakati kuhusu nadharia za kijeshi kuanzia mwanzo wa vita katika bahari kati ya Athens na Sparta hadi sasa. Lengo ni kuweka uhusiano kati ya Malengo ya Taifa kisiasa na namna ambayo mbinu zake za jeshi zinakuwa mahususi kutumika ili kufanikisha malengo yaliyokusudiwa (Ushindi).

Kozi ya pili ya Usalama wa Taifa katika Maamuzi imewekwa kwa ajili ya kuwasaidia watendaji wakuu katika jeshi na wananchi kukabiliana na hoja za kisiasa, kiuchumi, na kijeshi katika kufanya maamuzi sahihi kwenye masuala ya Usalama wa Taifa.

Kozi ya tatu ya kuunganisha operesheni za kijeshi inawasaidia wakuu wa taasisi za kijeshi kutafsiri mikakati ya kijeshi na hasa ya kikanda katika vita vya majini.

Karibu nusu ya wanafunzi wanaotoka Marekani ni maofisa kutoka jeshi, vikosi vya anga, majini, ulinzi wa mwambao na katika meli na kampuni na wakala wa ulinzi binafsi.

Uzoefu huo wa kazi na elimu kubwa ya ofisa huyo wa Marekani ulimfanya mwenyekiti wa CUF, Prof Ibrahim Lipumba kutokuwa na wasiwasi na ripoti ya Delly kwenda Ikulu ya Marekani.

“Delly hana sababu ya kumzulia Hoseah. Ni mzoefu na anajiamini katika kazi zake; haya ya kusema kwamba nimenukuliwa vibaya, ni ujanja ujanja wa kulindana tu,” alisema Profesa Lipumba ambaye alisomea shahada yake ya uzamili, akijikita katika uchumi kwenye Chuo Kikuu cha nchini Marekani.

“Yale yaliyoandikwa katika mtandao wa Wikileaks na baadaye kuchapishwa katika gazeti la The Guardian la Uingereza ni ya kweli ya Dk Hoseah na yale ya kukanusha ni ya kulindana.”

Prof Lipumba alidai kuwa ni kweli Rais Kikwete hayuko tayari hata siku moja kuona rais wa serikali ya awamu ya tatu, Benjamin Mkapa au waziri mkuu wake, Frederick Sumaye wakisimamishwa mahakamani kujibu tuhuma za ufisadi.

Alisema mambo hayo yanafanana kabisa na yaliyoandikwa katika gazeti hilo mwaka 2007 kwamba Hoseah anatembea na mlinzi mwenye silaha kutokana na kuhofia usalama wake.

“Jambo la msingi ambalo tunaliona hapa ni kwamba tuna udhaifu mkubwa katika uongozi na viongozi hawana utashi na ujasiri wa kupambana na rushwa... Hoseah na hata Kikwete hawawezi kupambana,” alisemai.

“Fedha ile (dola 12.4 milioni alizolipwa Shailesh Vithlani katika ununuzi wa rada) haina mjadala kuwa ni rushwa, ni rushwa ambayo alilipwa Vithlani kifisadi kufanikisha zabuni ya uuzaji wa rada kwa serikali ya Tanzania.”

Wakili wa siku nyingi nchini, Profesa Abdallah Safari alisema kuna uwezekano mkubwa kuwa taarifa iliyotolewa na mtandao huo ni ukweli.

"Kuamini utetezi wa Dk Hoseah ni vigumu kutokana na mwenendo wake," alisema Profesa Safari. "Alijaribu kumsafisha (mwanasheria na mbunge wa Bariadi Magharibi) Andrew Chenge katika kashfa ya rada.
“Amekuwa akitofautiana na ripoti mbalimbali mpaka za bunge kama ile ya Richmond. Kwa hiyo CCM ni watu wasioaminika na serikali yao... wana mambo yao bwana.”

Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Bashiru Ally alitazama suala hilo katika sura tatu, akielezea sura ya kwqanza kuwa ni nchi za Kiafrika kuanzisha taasisi zisizo huru na zinazoendeshwa kwa kutegemea msaada wa wahisani, akitoa mfano wa Takukuru.

“Hata ukisoma hiyo taarifa kwa umakini kwenye mtandao, utona kabisa kuwa Dk Hoseah alikuwa anajipendekeza kwa ajili ya kulinda ufadhili,” alisema Bashiru.

Alisema endapo Takukuru ingekuwa ni taasisi huru na inayojitegemea kwa kila kitu, basi kusingekuwa na sababu ya mkurugenzi wake kuzungumza na Wamarekani.

Katika mtazamo wake wa pili, Bashiru alisema wasomi, wanahabari na wanasiasa wana kazi kubwa ya kuangalia lengo la mtandao huo kufichua habari kama hizo zinzolihusu bara la Afrika na Asia.

“Lazima tujiulize kwa nini hizi siri zinafichuliwa wakati huu/ kwa nini Marekani na nchi kama Uganda, Iraq na Tanzania; kwa nini hakuna siri za Marekani na nchi nyingine tajiri kusema ni jinsi gani wanavyopanga kutugandamiza,” alisema Bashiru.

Kwa sura ya tatu, Bashiru alisema inakuwa vigumu kwa sasa kuangalia hatima ya mapambano ya rushwa, akisema ni lazima mtu ajitoe mhanga katika vita ya rushwa na kwamba kama hakuna dhamira ya kweli, huwezi kupambana.

“Dk Hoseah amekanusha baadhi ya mambo kwa hiyo labda tusubiri wamarekani wenyewe watuambie kama wamemlisha maneno, lakini kweli kwenye mapambano ya rushwa lazima mambo ya kutishiana maisha yawepo kwa sababu yanahusu watu wazito,” alisema Bashiru.

Mkurugenzi mtendaji wa taasisi isiyo ya kiserikali ya kukuza demokrasia nchini Agenda Participation 2000, Moses Kulaba alisema mtandao huo umefungua macho ya Watanzania.

Alisema siri zilizofichuliwa zimekuwa uthibitisho wa masuala ambayo Watanzania walikuwa wakiyawaza kwa muda mrefu.

“Mimi mwenyewe nimeusoma ule mtandao, bado kuna mengi ni mapema mno kwa Dk Hoseah kuanza kukanusha,” alisema Kulaba.

Hussein Kauli
Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kitivo cha Uchumi, Adolf Mkenda alimtaka Dk Hoseah ajiuzulu iwapo ni kweli alimuelezea Rais Kikwete kuwa hapendi vita dhidi ya rushwa.

Mkenda alisema kitendo cha Dk Hoseah kueleza mambo ya ndani kwa maofisa wa ubalozi wa Marekani wakati anajua yeye anawajibika kwa serikali ni ukiukwaji wa maadili ya kazi yake na hivyo anapaswa kuwajibika kwa kujiuzulu.

“Ni jambo la ajabu sana kwa Dk Hoseah kufanya kitendo hicho, kama taarifa hizi ni za kweli inabidi ajiuzulu mwenyewe kwani hafai kuendelea kuiongoza Takukuru” alisema Mkenda na kuongeza kuwa iwapo atajiwajibisha, serikali haina budi kumchukulia hatua.

Mkenda pia alieleza kuwa kama Rais Kikwete hapendi sheria ichukue mkondo wake katika vita dhidi ya rushwa, amekiuka katiba.


source mwananchi

Thamani ya Shilingi ya Tanzania yapanda

Sunday, December 19, 2010 / Posted by ishak / comments (0)


Thamani ya Shilingi ya Tanzania imepanda mfululizo kwa muda wote wa wiki mbili zilizopita tokea Desemba 3 Mwaka huu ukilinganisha na Dola ya Kimarekani.
Kwa mujibu wa takwimu zinazotolewa kila siku na Benki Kuu ya Tanzania (BoT), kiwango cha kubadilisha fedha Desemba 2, kilikuwa Shilingi 1,487.55 kwa Dola moja, lakini Desemba 3, kilishuka na kufikia Shilingi1,485.23 upungufu wa shilingi 2.32.
Hadi kufikia Desemba 10, Dola ilibadilishwa kwa shilingi 1,477.22, pungufu kwa shilingi 8.01 ikilinganishwa na kiwango cha ubadilishanaji wa shilingi kwa dola wa Desemba 3 uliokuwa shilingi 1,485.23.
Kuanzia Desemba 13 hadi jana thamani ya Shilingi ilipanda kwa kasi kubwa ambapo Desemba 13 dola ya Kimarekani ilibadilishwa kwa Shilingi1,466.23, Desemba 14 ilibadilishwa kwa Shilingi 1,455.72, Desemba 15 ilibadilishwa kwa Shilingi 1,443.39 na jana dola ilibadilishwa kwa Shilingi1,432.42.
Hivyo takwimu hizi za Bot zinamaanisha kuwa thamani ya fedha yetu imeimarika ukilinganisha na dola ya Kimarekani kwa kipindi hiki cha wiki mbili zilizopita.
Kupanda huku kwa thamani ya shilingi mfululizo unakinzana na namna ilivyoporomoka kwa haraka mwanzoni mwa Agosti wakati harakati za uchaguzi zilipoanza hadi kura zilipopigwa na kuendelea hivyo hadi mwanzoni mwa mwezi huu.

source nipashe

ray ,kanumba watua kigali ................

Thursday, December 16, 2010 / Posted by ishak / comments (0)





kama unavyowaona katika kiwanja cha ndege walipowasili na pia wakitembezwa katika mji wa kigali na kupokewa na mashabiki wa film za kibogo...............


source newtimes

Maalim Seif ataka kusaidiwa mzigo

Sunday, December 12, 2010 / Posted by ishak / comments (0)


KATIKA hali inayoashiria kuelemewa na mzigo wa majukumu, Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar, Seif Sharif Hamad, ambaye pia ni Katibu Mkuu wa CUF, amekiomba chama chake, kumtafuta mtu wa kumsaidia katika nafasi hiyo, wakati kikisubiri uchaguzi wake.

Rai hiyo imekuja huku Katibu Mkuu Msaidizi wa CUF, Juma Haji Duni, akiwa ameteuliwa kuwa Waziri wa Afya na Utabibu katika Serikali ya Umoja wa Kitaifa Zanzibar.

Uteuzi huo umefanywa na Rais wa Zanzibar, Dk Ali Mohamed Shein.

Maalim Seif alitoa kauli hiyo mbele ya Mwenyekiti wa CUF, Profesa Ibrahim Lipimba katika kikao cha Baraza Kuu la chama hicho, kilichofanyika jana jijini Dar es Salaam.

Katika kikao hicho, mtendaji huyo wa CUF pia alilitaka baraza kujipanga kwa uchaguzi mkuu ujao.

Maalim Seif alisema mtu atakayepata nafasi hiyo ya kumsaidia kwa muda lazima atambue kuwa nafasi hiyo itakuwa bado mikononi mwake (Seif) hadi atakapoyaachia rasmi majukumu ya umakamu wa Rais wa Zanzibar.

"Katibu mkuu atakayepata nafasi ya kuteuliwa, ajue yeye si Katibu Mkuu wa CUF, katibu mkuu nitabaki kuwa ni mimi hadi nitakapoiachia nafasi hii rasmi kwa kufuata utaratibu,"alisema Maalim Seif.

Alimuomba mwenyekiti kwa kushirikiana na baraza, kumsaidia katika kumtafuta au kumpendekeza mtu atakayemsaidia katika nafasi hiyo.

Katika kikao hicho, kiongozi huyo pia alimshukuru Rais wa Serikali ya Umoja wa Kitaifa Zanzibar, Dk Shein kwa kuweka uwiano mzuri katika uteuzi wa Baraza la Mawaziri na kwamba uteuzi huo, utaleta mabadiliko makubwa kwa wananchi wa Zanzibar.

Alisema CUF imepata mafanikio makubwa katika uteuzi huo kwa kuwa umepata nafasi ya kuongoza nchi na kwamba kwa sasa Zanzibar inaongozwa na vyama vya CCM na CUF tofauti na miaka ya nyuma ambapo nchi ilikuwa ikiongozwa na chama kimoja.

"Chama chetu ni miongoni mwa vyama viwili vinavyoongoza serikali, kwa hiyo tujivunie ushindi wetu kwani tumetimiza malengo ya CUF ya kushika madaraka ya nchi, tangu tukiunde tumejaribu mara tatu tukashindwa lakini mwaka huu tumeweza,"alisema.

Hata hivyo, alisema ushindi huo ni changamoto kwa CUF na kwamba wote waliopata uongozi wanapaswa kubeba majukumu na kuhakikisha kuwa wanawatumikia wananchi bila kubagua.

Alisema uteuzi wa mawaziri nane kutoka chama hicho ni mkubwa sana hasa ikizingatiwa kuwa Rais Dk Shein, alikuwa na uwezo wa kufanya lolote katika uteuzi huo.

"Mimi ni Makamu wa Kwanza wa Rais, nitamsaidia Rais wangu kufanya kazi kwa bidii kwa kushirikiana na mawaziri wote bila kuangalia kama ni wa CCM au CUF, nina hakika sote kwa pamoja tutaleta mabadiloko,"alisema.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa CUF (Lipumba) alimpongeza Maalim Seif kwa kuonyesha ukomavu wa siasa wakati wa kusubiri matokeo ya kura na baada ya kutangazwa kwa kutoa hotuba ya kihistoria tofauti na matarajio ya watu weng.

Alisema baadhi ya waty walidhani kuwa kauli yake ingeleta maafa.

"Tunampongeza kwa kuhakikisha kuwa maslahi ya wananchi wa Zanzibar yanakuwa mbele badala ya maslahi binafsi kuchukua nafasi. Pia tunampongeza Dk Shein kwa ushirikiano aliotuonyesha katika kuunda baraza lake la mawaziri," alisema.

Alifafanua kuwa mafanikio ya CUF ni matokeo ya maridhiano mazuri yaliyofanywa na Katibu mkuu wa chama na Rais mstaafu wa Zanzibar, Abeid Amani Karume.


Alisema kuwa CUF imefungua njia, ili kwa pamoja wannchi wa Zanzibar, waweze kutatua matatizo yao na kuondokana na umaskini.

source mwananchi

Zitto adai amelishwa sumu

Sunday, December 12, 2010 / Posted by ishak / comments (0)


MBUNGE wa Kigoma Kaskazini, Zitto Kabwe ambaye jana aliruhusiwa kutoka katika Hospitali ya Aga Khan ya jijini Dar es Salaam alikolazwa kwa matibabu ya tumbo amedai kuwa matatizo hayo aliyapata baada ya kula chakula chenye sumu.“Namshukuru Mungu naendelea vizuri na nimesharuhusiwa kutoka hospitali, madaktari wameniambia ilikuwa food poisoning (chakula chenye sumu),” alisema Zitto.

Zitto ambaye hakuweza kueleza chakula hicho alikuwa wapi na kina sumu ya aina gani, alisema kuwa baada ya kugundua tatizo hilo, madaktari walimtaka kuwa makini na vyakula anavyokula.

“Sumu gani nimekula na ni wapi, mimi nadhani sio story (habari). Cha msingi kwa sasa naendelea vizuri na nimetakiwa kuwa makini na vyakula ninavyokula,” alisema Zitto.

Hata hivyo, kauli hiyo ya Zitto inapingana na madaktari wake waliosema kuwa mbunge huyo kupitia tiketi ya Chadema, alikuwa anasumbuliwa na mchafuko wa kawaida wa tumbo.

“Alikuwa anasumbuliwa na Gastro enteritis (mchafuko wa tumbo), tatizo hili linaweza kusababishwa na bacteria, virusi katika chakula, au kama chakula hakijapikwa vizuri,” alisema Dk Mustafa Bapumia.

Zitto alilazwa hospitalini hapo tangu Disemba 9 mwaka huu saa 3:00 usiku, baada ya kutoka kwenye mkutano wa ndani wa chama chake uliofanyika Bagamoyo mkoani Pwani ambako alivuliwa cheo cha Naibu Kiongozi wa Kambi ya upinzani bungeni.

Kuhusu hatua ya chama hicho kumvua Zitto wadhifa wake wa unaibu kiongozi wa upinzani bungeni, alisema kwa sasa bado hawezi kuzungumzia suala hilo kwa sababu hajapata taarifa rasmi kutoka chama chake mbali na kusoma suala hilo kwenye vyombo vya habari.

Hata hivyo, alieleza hakuwahi kuomba kupewa wadhifa huo, kwa hiyo endapo watu waliomwona anafaa kufanya kazi na kumpa wadhifa huo, wakiamua kumnyang’anya siyo tatizo kubwa kwake.

“Kwa sasa nadhani suala la afya yangu ndiyo muhimu zaidi. Ngoja kwanza nitoke hapa na afya yangu iimarike na kama kutakuwa kuna sababu ya mimi kuzungumza nitazungumza,” alisema Zitto:

“Lakini ikumbukwe kuwa mimi sikuwahi kuomba wadhifa huu…, kwa hiyo kama watu walionipa wameamua kunibadilishia, mimi sidhani kama kuna tatizo.”

Mwenyekiti wa chama hicho, Freeman Mbowe aliupolizwa na Mwananchi Jumapili juu ya Zitto kuvuliwa uongozi bungeni alisema kuwa chama kitatoa taarifa baadaye.

Katika hatua nyingine Mbunge wa Mpanda Mjini, Said Amur Arfi aliyekuwa amelazwa katika Hospitali ya Aga Khan ya jijini Dar es Salaam, amesafirishwa kwenda India kwa matibabu zaidi.

Arfi aliliambia Mwananchi Jumapili kuwa madaktari waliokuwa wakimtibu wamemwambia kuwa mfuko wake wa nyongo una mawe hivyo anahitaji kufanyiwa upasuaji.

“Nilikuja hapa kwa sababu nilikuwa nasumbuliwa na maumivu makali ya tumbo, nilitoka Mpanda Disemba 2, mwaka huu kuja kwenye semina lakini kutokana na maumivu ya tumbo nilienda Hospitali ya Regency na baada ya kupigwa ultrasound nilielezwa kuwa nina tatizo la uvimbe kwenye maini,” alisema Arfi.

Alisema alivyokwenda katika Hospitali ya Aga Khan alielezwa kuwa ana tatizo jingine la mawe kwenye mfuko wa nyongo na kuwa inabidi afanyiwe upasuaji.

“Naishukuru serikali kupitia ofisi ya Bunge kunipeleka India kwa matitabu zaidi,” alisema Arfi.

Hata hivyo, alisema bado hajaelezwa hospitali anayokwenda kutibiwa na kuwa, taarifa zote hizo anazo muuguzi wa serikali atakayesafiri naye.
Wakati huohuo, Mtangazaji wa Televisheni ya Channel Ten, Cyprian Musiba, anadaiwa kuwekewa sumu kwenye chakula na kufanya alazwe hospitalini kwa matibabu.

Musiba alilazwa katika kituo cha Afya cha Ebrahim Haji kilichopo jijini Dar es Salaam juzi mchana akiwa hajitambui.

Mmoja wa madaktari wa hospitali hiyo, Dk Ramadhani Ali aliliambia Mwananchi Jumapili kuwa Musiba alifikishwa katika hospitali hiyo akiwa anasumbuliwa na tumbo lakini, baada ya kupata matibabu, afya yake iliimarika na jana mchana aliruhusiwa kutoka hospitalini.

“Anaendelea vizuri kwa kweli na amesharuhusiwa” alisema Dk Ali huku akisita kueleza tatizo la lililokuwa linamsumbua Musiba.

Mke wa Musiba ambaye hakujitambulisha alisema kuwa kabla ya Musiba kuruhusiwa mmoja wa madaktari wa HospitaliI hiyo waliwaeleza kuwa Musiba alikula sumu iliyokuwa katika chakula.

“Tumeruhusiwa muda si mrefu ila daktari amesema Musiba alijisikia vibaya kwa kuwa alikuwa amekula sumu iliyokuwa katika chakula,”alisema mke wa Musiba.

Musiba ambaye mara nyingi hutangaza habari za michezo na burudani aliliambia Mwananchi Jumapili kuwa juzi hali yake ilikuwa mbaya na kuongeza kuwa alipelekwa katika hospitali hiyo kwa ajili ya matibabu.

“Hali yangu ilikuwa mbaya sana nilikuwa wa kufa tu ndugu yangu, ila namshukuru mungu naendelea vizuri, ila daktari hapa hospitali amenieleza kuwa nilikula sum,” alisema Musiba.

Habari zaidi zilidai kuwa Musiba alianza kupata matatizo ya tumbo saa kadhaa baada ya kula chakula katika hoteli moja iliyopo karibu na ofisi za Channel Ten

source mwananchi

Barafu inatabiriwa kuongezeka UK...........

Sunday, December 05, 2010 / Posted by ishak / comments (0)



HALI ILIVYO UINGEREZA SASA

Kitabu cha Mafunzo ya Wizi

Tuesday, November 30, 2010 / Posted by ishak / comments (0)


Mwizi wa nchini Japan ambaye kutokana na kufanya wizi kwa mwaka alikuwa akijiingizia kiasi cha pesa sawa na Tsh. Milioni 540 ametoa kitabu cha kuelezea jinsi ya kuiba kwenye majumba ya watu bila kugundulika, kitabu hicho kimekuwa gumzo nchini Japan na kinanuliwa kwa wingi.
Mwizi wa nchini Japan, Hajime Karasuyama kutokana na utaalamu wake wa kuiba kwenye majumba ya watu, ametoa kitabu kinachoelezea jinsi ya kuiba kwa ustadi mkubwa bila ya kugundulika.

Kitabu chake kinachoenda kwa jina la "Kazi: Mwizi, Kipato Kwa mwaka: Yen Milioni 30", kimekuwa gumzo nchini Japan na kimekuwa kikinunuliwa kama njugu.

Wachapishaji wa kitabu hicho Futabasha Publishing wamesema kuwa nakala za mwanzo za kitabu hicho zipatazo 10,000 zimenunuliwa zote ndani ya siku 10 baada ya kitabu hicho kuzinduliwa.

Katika kitabu hicho, Karasuyama anaelezea jinsi ya kufungua vitasa vya milango ya aina yoyote ile kwa muda mfupi na bila ya ufunguo na jinsi ya kuvunja madirisha ya vioo bila ya kusababisha kelele.

Karasuyama ameelezea pia jinsi alivyokuwa akitumia lensi kuangalia ndani ya nyumba kwa kupitia kwenye tundu la funguo.

Mbali ya wizi wa majumbani, Karasuyama pia amelezea pia njia za kufanya utapeli na kuwaacha watu kwenye mataa.

Karasuyama alisema kuwa kutokana na wizi alikuwa akijiingizia kitita kinono kwa mwaka zaidi ya Tsh. Milioni 540.

"Tunapoingia ndani ya nyumba, sisi wezi huwa tunajua wapi watu huficha pesa zao", alisema Karasuyama alipokuwa akiongea na jarida la Shukan Taishu kuhusiana na kitabu chake ambacho kimeambatanisha maneno ya "Usijaribu kuniiga" kwenye ukurasa wake wa kwanza.

Wachapishaji wa kitabu hicho kinachouzwa Yen 1,200 sawa na Tsh. 20,000 wamekanusha madai kuwa kuchapishwa kwa kitabu hicho kutapelekea baadhi ya watu kugeuka wezi kwa kuiga staili za wizi za Karasuyama.

Wachapishaji hao wamesema kuwa kitabu cha Karasuyama kitawawezesha watu kujifunza njia zinazotumiwa na wezi hivyo kuweza kuzilinda vyema nyumba zao.

source nifahamishe