Jambazi Anapowatumia Polisi Picha Yake...

Sunday, November 08, 2009 / Posted by ishak /


Jambazi anayetafutwa na polisi kila kona nchini Uingereza amewatumia polisi picha yake mpya aliyopiga akiwa mbele ya gari ya polisi baada ya kuchukizwa na picha yake ambayo polisi waliitoa kwenye magazeti wakiomba wananchi wawasaidie kumnasa.
Jambazi Matthew Maynard mwenye umri wa miaka 23 hakuipenda picha yake iliyotolewa kwenye magazeti na aliamua kuwatumia polisi picha yake mpya aliyopiga akiwa mbele ya gari la polisi.

Polisi katika mji wa Swansea walitoa tangazo la kutafutwa kwa Matthew katika gazeti la Evening Post la mji huo. Tangazo hilo liliambatana na picha yake ndogo inayoonyesha sura yake.

Baada ya picha hiyo kuchapishwa kwenye gazeti hilo, Matthew ambaye pamoja na wenzake wanne wanatafutwa na polisi kwa makosa ya ujambazi, alipiga simu kwenye ofisi ya gazeti hilo akisema kuwa hajaipenda picha yake iliyotolewa kwenye gazeti hilo na aliwaahidi atawatumia picha nyingine waiweke kwenye gazeti lao.

Wakati waandishi wa gazeti hilo wakiwa hawaamini kama kweli atawatumia picha yake, Matthew alitumia simu yake kuwatumia picha yake aliyopiga akiwa mbele ya gari la polisi akiwa amevaa jaketi linalofanana na majaketi wanayopenda kuvaa mapolisi.

Picha yake hiyo ilitolewa juzi kwenye ukurasa wa mbele wa gazeti la Evening Post.

Jana polisi wa Swansea walimshukuru Matthew kwa kuwasaidia polisi katika harakati zao za kumtia mbaroni.

"Anajiona mjanja sana kwa kujionyesha namna hii, tutamnasa muda si mrefu", alisema afisa mmoja wa polisi.

"Watu wote wa Swansea wanajua sasa jinsi alivyo na watatupa taarifa zitakazofanikisha kukamatwa kwake".

"Kama ana akili angejisalimisha mwenyewe polisi sasa kwakuwa hana pa kukimbilia tena", alimalizia kusema afisa huyo.

source.nifahamishe.com

0 comments:

Post a Comment