Ili Kupinga Obama Kuwa Rais, Alichoma Moto Kanisa la Watu Weusi

Saturday, June 19, 2010 / Posted by ishak / comments (0)


Mwanaume mmoja wa nchini Marekani anakabiliwa na kifungo cha miezi 108 jela baada ya kukiri kulichoma moto kanisa la watu weusi ili kupinga Barack Obama kuwa rais mweusi wa Marekani.
Benjamin Haskell, 23, wa Massachusetts nchini Marekani amekiri kosa lake la kulichoma moto kanisa la Wamarekani weusi ili kupinga kuchaguliwa kwa Barack Obama kuwa rais wa kwanza mweusi wa Marekani.

Benjamin alikiri jana kulichoma moto kanisa la Macedonia Church of God in Christ mnamo novemba 5 mwaka 2008, ikiwa ni ndani ya masaa machache baada ya Obama kuchaguliwa kuwa rais.

Benjamin alilimwagia petroli kanisa hilo kabla ya kulipiga kiberiti na kuliteketeza.

"Leo tunatoa ujumbe kuwa watu wanaofanya uhalifu kwa sababu za chuki, watachunguzwa na baadae ya kushtakiwa", alisema Carmen Ortiz mwanasheria mkuu wa Massachusetts.

Benjamin huenda akahukumiwa kwenda jela miezi 108 (miaka 9) baada ya kukiri kosa lake la kuhatarisha maisha ya waumini 300 wa kanisa hilo na kuliharibu jengo la kidini kwasababu ya chuki zake ubaguzi wa rangi.

source nifahamishe

Wivu Wapelekea Amchome Moto Mpenzi Wake

Saturday, June 19, 2010 / Posted by ishak / comments (0)


Kutokana na wivu mwanamke mmoja nchini Marekani alimchoma moto mpenzi wake na kisha kujichoma moto na yeye mwenyewe na kutokana na moto huo nyumba ilishika moto na kupelekea vifo vya watu wengine watatu.
Agnes Bermudez, 50, anatuhumiwa kumuua mpenzi wake William Salazar, 32, katika tukio la kutisha lililotokea siku ya akina baba duniani mwaka 2008.

Agnes ambaye hivi sasa kesi yake inaendelea mahakamani, alimchoma moto mpenzi wake huyo na kisha yeye mwenyewe alijipiga kibiriti.

Agnes hakufariki kutokana na moto aliouanzisha lakini aliungua vibaya sura yake kiasi cha kumfanya asitambulike.

Sababu ya Agnes kumchoma moto mpenzi wake ni wivu wa kimapenzi. Agnes alimshutumu Salazar kuwa anatembea na mwanamke mwingine nje.

Video ya tukio hilo imetolewa mahakamani kama ushahidi wa tukio hilo la kusikitisha.

Video inamuonyesha Agnes na Salazar wakitoka nje ya nyumba yao wakikimbilia kwenye duka lililopo chini ya jengo lao.

Salazar anaonekana akikimbia kuingia ndani ya duka akitafuta maji wakati Agnes alilala chini mbele ya duka hilo huku akiungua na moto.

Wasamaria wema walifanikiwa kuwamwagia maji na kuokoa maisha yao hata hivyo Salazar alifariki siku nne baadae hospitalini.

Moto ulioanzishwa na Agnes ulishika pia nyumba zingine zilizopo kwenye jengo hilo na kupelekea vifo vya watu watatu.

Mke Amuua Mume Kwasababu ya Kombe la Dunia

Saturday, June 19, 2010 / Posted by ishak / comments (0)

Kombe la dunia linaloendelea nchini Afrika Kusini limekuwa sababu ya kifo cha mwanaume mmoja nchini humo ambaye alifariki baada ya kupigwa na mkewe na watoto wake wakati alipolazimisha kuangalia mechi kwenye TV wakati mkewe na watoto wake walitaka kuangalia nyimbo za dini.
David Makoeya mwenye umri wa miaka 61 hakutaka kuikosa mechi ya jumapili iliyopita kati ya Ujerumani na Australia.

Mke wake na watoto wake wao walitaka kuangalia programu ya nyimbo za dini za kikristo kwenye luninga.

Polisi wanasema kuwa Makoeya alikuwa akigombania remote control na familia yake ili aweze kuangalia mechi ya kombe la dunia.

Familia yake walikataa kubadilisha channel ya mambo ya dini waliyokuwa wakiiangalia na hapo ndipo mzozo ulipoanzia.

"Alisema, Hapana nataka kuangalia mpira", msemaji wa polisi Mothemane Malefo alisema.

Huku akiwa na hasira, Makoeya alinyanyuka na kuelekea kwenye TV ili aweze kubadilisha channel lakini hakufika mbali kwani mkewe na watoto wake walianza kumshushia kipigo.

Mke wa Makoeya mwenye umri wa miaka 68, Francina, akishirikiana na mtoto wake wa kiume Collin mwenye umri wa miaka 36 na binti yake Lebogang mwenye umri wa miaka 23 walimshushia kipigo cha nguvu baba yao.

"Inaonekana walikipigiza kichwa chake kwenye ukuta, walipiga simu polisi baada ya kumjeruhi vibaya sana... wakati polisi wanafika eneo la tukio, Makoeya alikuwa ameishafariki", alisema Malefo.

Mke wa Makoeya na wanae ambao wanaishi kwenye kijiji cha Makweya, walitiwa mbaroni jumapili usiku.

Binti yake aliachiwa kwa dhamana ya dola 200 wakati mkewe na mtoto wake wa kiume wanaendelea kunyea debe rumande.

Ndugu wa familia hiyo wamesikitishwa na kifo cha Makoeya wakisema kuwa Makoeya hakuwa mtu mwenye vurugu alikuwa mtulivu na mwenye furaha kwa familia yake.

Kifo cha Makoeya kimetokea ikiwa ni siku chache baada ya watoto wawili kufariki nchini Uganda kutokana na moto baada ya wazazi wao kuwaacha wakiwa wamelala na kwenda kuangalia mechi ya kombe la dunia.

source nifahamishe

Azamia Jela Baada ya Kuona Maisha Magumu Uraiani

Saturday, June 19, 2010 / Posted by ishak / comments (0)


Mwanaume mmoja wa nchini Msumbiji ambaye alitoka jela kwa msamaha wa rais baada ya kukaa jela miaka mitano, amevunja ukuta wa fensi ya jela na kurudi gerazani baada ya kuona maisha ya uraiani ni magumu.
Camilo Antonio, 28, aliamua kurudi gerezani mwenyewe baada ya kugundua kuwa hayapendi tena maisha ya uraiani.

Camilo alitumikia miaka mitano jela kati ya 10 aliyohukumiwa kwa kumuua baba yake wa kambo, alitolewa jela baada ya kupewa msamaha wa rais.

Camilo ambaye alitumikia kifungo chake katika jela ya Manica iliyopo ukanda wa kati wa Msumbiji, alishindwa kustahamili maisha magumu ya uraiani na kuamua ni bora arudi jela.

Alishindwa kupata kazi na alikuwa na hofu familia ya baba yake wa kambo ingejaribu kumuua.

Camilo aliamua kuvunja sehemu ya ukuta wa jela ili aweze kuingia ndani. Alikamatwa na kushtakiwa kwa uharibifu wa mali za serikali na alihukumiwa kwenda jela mwaka mmoja.

"Kwajinsi ninavyoona jela kwangu ni sehemu salama kuliko sehemu zote", alisema Camilo kuliambia gazeti la Noticias la nchini Msumbiji.

"Sitaki kuishi jela maisha yangu yote lakini kwa wakati huu jela ni bora kuliko sehemu yoyote ile", alimalizia kusema Camilo.

Apanga Kumuua Osama Bin Laden kwa Jambia

Wednesday, June 16, 2010 / Posted by ishak / comments (0)


Raia mmoja wa Marekani alijaribu kufanya kile ambacho serikali yake imeshindwa kukifanya kwa miaka kadhaa kwa kuamua kwenda peke yake nchini Afghanistan kumsaka na kumuua Osama bin Laden akiwa na bastola, panga na jambia.
Mmarekani Gary Brooks Faulkner mwenye umri wa miaka 52 ametiwa mbaroni nchini Pakistan akiwa kwenye misheni yake ya kumsaka na kumuua kiongozi wa Al-Qaeda, Osama bin Laden.

Faulkner alitiwa mbaroni jumapili jioni akiwa kwenye harakati za kuvuka mpaka wa Pakistan kuingia Afghanistan ili kukamilisha nia yake ya kumuua Osama ambaye inasemekana amejificha kwenye milima iliyopo kwenye mpaka wa Afghanistan na Pakistan.

Alikamatwa akiwa na bastola moja, panga, jambia na vifaa vya kumwezesha kuona nyakati za usiku. Pia alikuwa na kitabu alichoandika mistari aliyoinukuu toka kwenye biblia.

Faulkner ambaye amebatizwa jina la "American Ninja" na magazeti ya Marekani anasumbuliwa na matatizo ya figo na shinikizo la damu, alikuwa amebeba dawa zake wakati wa safari yake hiyo ya kumsaka Osama.

Faulkner aliwasili nchini Pakistan juni 2 mwaka huu kama mtalii toka California, Marekani. Alipewa mlinzi wa kuongozana naye wakati wa utalii wake lakini alitoweka ghafla jumatatu ya wiki iliyopita na kuwafanya polisi waanze msako wa kumtafuta.

Alikutwa kwenye misitu iliyopo kilomita chache toka mpakani karibu na mji wa Nuristan wa nchini Afghanistan ambao unasemekana ni ngome ya Taliban nchini Afghanistan.

Faulkner aliwaambia polisi kuwa alikuwa kwenye misheni ya kumsaka na kumuua Osama bin Laden.

Alipoulizwa kama anafikiria ana uwezo wa kumkamata Osama, Faulkner aliwaambia polisi "Mungu yuko pamoja nami, nina imani nitamuua Osama bin Laden".

Faulkner aliwaambia polisi kuwa aliamua kwenda mwenyewe kumuua Osama baada ya kuchukizwa na shambulizi la kigaidi la septemba 11, 2001.

Serikali ya Marekani imekuwa ikimsaka Osama bin Laden kwa matukio ya kigaidi duniani na kichwa cha Osama bin Laden kimetengewa zawadi ya dola milioni 25 kwa mtu atakayetoa taarifa za kufanikisha kukamatwa kwake.

source nifahamishe

Sanamu la Yesu Lapigwa na Radi, Lateketea Kwa Moto

Wednesday, June 16, 2010 / Posted by ishak / comments (0)


Sanamu kubwa sana la Yesu lilikowa likijulikana kama 'Mfalme wa Wafalme' ambalo lilikuwa kivutio kikubwa cha watalii mjini Ohio nchini Marekani limepigwa na radi na kuteketea kwa moto.
Sanamu hilo maarufu lenye urefu wa mita 19 na upana wa mita 12 liliteketea kwa moto baada ya kupigwa na radi jumatatu usiku, taarifa ya polisi ilisema.

Sanamu hilo lililokuwa likijulikana kama "King of Kings" lilikuwa ni miongoni mwa vivutio vya watalii kusini magharibi mwa Ohio kuanzia mwaka 2004 lilipowekwa pembeni ya barabara ya kuu inayokatiza mbele ya kanisa la Kianglikana Monroe.

Taarifa ya polisi ilisema kuwa sanamu hilo liliteketea kwa moto jumatatu usiku kabla ya moto huo kudhibitiwa na maafisa wa zimamoto. Hakuna aliyejeruhiwa katika tukio hilo.

Sanamu hilo liligharimu dola 250,000 kulitengeneza na kutokana na ukubwa wake watu wengi wanaopita kwenye barabara ya Interstate 75 walikuwa wakisimama kwa muda mbele ya kanisa ili kupata taswira za sanamu hilo.

source nifahamishe

Zawadi ya Kiongozi Bora Afrika Yakosa Mshindi

Wednesday, June 16, 2010 / Posted by ishak / comments (0)


Kwa mwaka wa pili mfululizo mshindi hajapatikana kwaajili ya zawadi ya dola milioni 5 ya kiongozi bora wa Afrika ambaye ameonyesha mfano wa uadilifu katika uongozi na serikali ya kidemokrasia.
Wadhamini wa tuzo ya kiongozi bora wa Afrika wamesema kuwa mwaka huu pia wameshindwa kumpata kiongozi wa nchi aliyeonyesha mfano wa uongozi bora na serikali ya kidemokrasia.

Washindi wa tuzo ya kiongozi bora wa Afrika hupewa zawadi ya dola milioni 5 ndani ya kipindi cha miaka 10 na baada ya miaka 10 kuisha hupewa dola laki mbili kila mwaka kwa miaka yote ya maisha yao iliyobaki.

Mo Ibrahim, mfanyabiashara bilionea aliyezaliwa nchini Sudan ndiye aliyeanzisha tuzo hizo mwaka 2006 ili kuwapa moyo viongozi wa Afrika kuongoza serikali zao kwa misingi bora ya uongozi.

Kamati huru ya watu saba ikiongozwa na katibu mstaafu wa umoja wa mataifa, Kofi Annan, ilikutana tena jumamosi lakini ilishindwa kumchagua mshindi.

Kamati hiyo pia mwaka jana ilishindwa kumchagua kiongozi yoyote wa Afrika kushinda tuzo hiyo.

Tuzo hiyo hutolewa kwa viongozi wa Afrika waliochaguliwa kidemokrasia ambao wameachia madaraka ndani ya miaka mitatu iliyopita.

"Sifa za viongozi bora zilizowekwa ziko juu na kila mwaka idadi ndogo ya viongozi wenye sifa hupatikana. Kwahiyo kuna uwezekano miaka mingine hatapatikana mshindi", alisema Mo Ibrahim.

Hadi sasa ni viongozi wawili tu wa Afrika ambao wamezawadia tuzo hiyo, rais mstaafu wa Botwana, Festus Mogae na rais mstaafu wa Msumbiji, Joaquim Chissano. Rais wa zamani wa Afrika Kusini, Nelson Mandela alipewa tuzo maalumu ya heshima mwaka 2007.

source nifahamishe

Watoto Wafariki Wakati Baba na Mama Wakiangalia Kombe la Dunia

Wednesday, June 16, 2010 / Posted by ishak / comments (0)


Watoto wawili wamefariki dunia nchini Uganda kutokana na moto ulioitekeza nyumba yao wakati wazazi wao walipoenda kwa jirani mwenye televisheni kuangalia kombe la dunia.
Polisi mjini Kampala nchini Uganda wamesema kuwa watoto wawili wamefariki kutokana na moto ulioitekeza nyumba yao wakati wazazi wao walipoenda kuangalia mechi ya kombe la dunia.

Polisi nchini Uganda wamewaonya wazazi kutowaacha watoto wao peke yao ndani ya nyumba wakati wanapoenda kuangalia mechi za kombe la dunia.

Watoto wawili wenye umri wa miaka 8 na 10 walifariki kwa moto katika wilaya ya Kayunga iliyopo magharibi mwa mji wa Kampala.

Afisa wa polisi wa Kayunga, Henry Kolyanga alisema kuwa watoto hao walifariki wakati nyumba waliyokuwa wamelala iliposhika moto.

"Mama na Baba wa watoto hao waliacha mshumaa ukiwaka ndani ya nyumba na walienda kuangalia mechi ya kombe la dunia kwa jirani mwenye televisheni", alisema afisa huyo wa polisi.

"Inasemekana kuwa panya aliugonga mshumaa na mshumaa huo uliangukia kwenye meza na kukiunguza kitambaa cha mezani na kusababisha moto mkubwa ulioitekeza nyumba yote", alimalizia kusema afisa huyo wa polisi.


source nifahamishe

Miaka 10 Jela Kwa Kumuua Dada Yake Aliyepata Mimba Nje ya Ndoa

Tuesday, June 15, 2010 / Posted by ishak / comments (0)


Mahakama nchini Jordan imemuondolea adhabu ya kifo aliyohukumiwa mwanaume aliyemuua dada yake baada ya kugundua amepata mimba kabla ya kuolewa. Mahakama imeamuru mwanaume huyo atumikie kifungo cha miaka 10 jela.
Mwanaume huyo mwenye umri wa miaka 24 alimuua dada yake mwenye umri wa miaka 26 kwa kumchomachoma na kisu tumboni mara 15 baada ya kugundua dada yake huyo amepata ujauzito kabla ya kuolewa.

Awali mahakama ya mjini Amman, Jordan iliamuru mwanaume huyo ahukumiwe adhabu ya kifo lakini jana mahakama iliamuru mwanaume huyo atumikie kifungo cha miaka 10 jela baada ya familia yake kumuombea msamaha mahakamani.

"Alimuua dada yake baada ya dada yake huyo kumwambia kuwa alifanya mapenzi na mwanaume ambaye alisafiri kwenda kufanya kazi nchini Saudi Arabia", alisema afisa wa mahakama ambaye hakutaka kutaja jina lake.

Taarifa ya mahakama ilisema kuwa mauaji hayo yalifanyika mwaka jana katika mji wa Karak wakati huo dada yake alikuwa na mimba ya wiki nne.

Kwa mujibu wa sheria za Jordan, mtu anayeua naye huuliwa lakini kwa mauaji yanayoitwa "Kulinda Heshima ya Familia" adhabu ya kifo huondolewa iwapo familia ya mwanamke aliyeuliwa itaiomba mahakama ipunguze adhabu kwa muuaji.

Wanawake 15 hadi 20 huuliwa kila mwaka nchini Jordan kwa staili hiyo hiyo ya kulinda heshima za familia ingawa serikali ya Jordan inafanya jitihada ya kuiondoa tamaduni hiyo potofu.

source nifahamishe

Marekani Yagundua Hazina ya Utajiri Afghanistan

Tuesday, June 15, 2010 / Posted by ishak / comments (0)


Marekani imegundua hazina ya madini yenye thamani kubwa nchini Afghanistan ambayo yanakadiriwa kuwa na thamani ya zaidi ya dola trilioni moja.
Msemaji wa Pentagon alisema kuwa utafiti wa wataalamu wa madini wa Marekani umeonyesha kuwa nchini Afghanistan kuna kiasi kikubwa sana cha madini ya thamani tofauti na ilivyokuwa ikijulikana awali.

Thamani ya madini kama vile niobium, lithium, chuma, dhahabu na kobalti ambayo yanapatikana kwa kiasi kikubwa nchini Afghanistan ni zaidi ya dola trilioni moja.

Maafisa wa Marekani waliliambia gazeti la New York Times la Marekani kuwa hazina ya madini yaliyopatikana nchini Afghanistan yanatosha kuubadilisha uchumi wa Afghanistan na kuigeuza Afghanistan kuwa mojawapo ya nchi zinazoongoza kwa uzalishaji wa madini duniani.

Rais wa Afghanistan, Hamid Karzai alisema mwanzoni mwa mwaka huu kuwa kiasi kikubwa cha madini kilichogunduliwa nchini humo kitaifanya Afghanistan itoke kwenye umaskini iwe miongoni mwa nchi tajiri duniani.

Aozeshwa Ng'ombe Aliyembaka, Azimia Wakati wa Harusi

Tuesday, June 15, 2010 / Posted by ishak / comments (0)


Kijana mmoja wa nchini Indonesia ambaye alilazimishwa kumuoa ng'ombe aliyembaka, alizimia wakati wa harusi yake na ng'ombe huyo.
Kijana Ngurah Alit mwenye umri wa miaka 18 alikamatwa kwenye kijiji chake cha Yeh Embang katika kisiwa cha Bali nchini Indonesia, akiwa uchi wa mnyama akifanya mapenzi na ng'ombe.

Alit alijitetea kuwa ng'ombe huyo ndiye aliyemtongoza yeye na kumvutia kufanya naye mapenzi.

Alit alidai kuwa aliamini kuwa ng'ombe huyo alikuwa ni msichana mrembo ambaye alikuwa akimfanyia mitego mbalimbali ili afanye naye mapenzi.

Pamoja na utetezi wake, Alit alilazimishwa amuoe ng'ombe huyo na harusi ya kitamaduni iliandaliwa.

Wakati polisi wakiwaweka waandishi wa habari mbali na eneo la harusi, Alit alizimia kabla ya kukabidhiwa rasmi 'mke' wake.

Hata hivyo Alit aligeuka mjane punde baada ya harusi baada ya bi harusi wake kuzamishwa kwenye bahari kama mojawapo ya imani za kijiji hicho.

Ili kusafishika na kitendo chake, Alit aliogeshwa kwenye ufukwe wa bahari.

Mkuu wa kijiji hicho alisema baada ya harusi hiyo kuwa kijiji sasa kimesafishika baada ya tukio hilo lililoleta aibu kwenye kijiji.


source nifahamishe

Watu Wafupi Wako Kwenye Hatari ya Kufa Kwa Magonjwa ya Moyo

Tuesday, June 15, 2010 / Posted by ishak / comments (0)


Utafiti uliofanywa kwa miaka 50 ukiwashirikisha watu milioni 3 umeonyesha ufupi ni tatizo na watu wafupi wako kwenye hatari ya kufariki kwa magonjwa ya moyo kulinganisha na watu warefu.
Baada ya miaka 50 ya utafiti wanasayansi wamegundua kuwa ufupi wa mtu ni mojawapo ya sababu zinazochangia watu kupata magonjwa ya moyo.

Utafiti huo ulionyesha kuwa watu wafupi wako kwenye hatari ya asilimia 50 zaidi ya watu warefu kupata magonjwa ya moyo.

Kwa wastani mtu alihesabika mfupi akiwa na urefu wa sentimeta 160.5 wakati mtu alihesabika mrefu alipokuwa na urefu wa sentimeta 173.9.

Utafiti huo ulionyesha usahihi kwa jinsia zote za kike na kiume ingawa kipimo cha urefu wa mwanaume na mwanamke kilikuwa tofauti.

Wanaume wafupi walitajwa kuwa na urefu chini ya sentimeta 165.4 wakati wanaume warefu walikuwa na urefu kuanzia sentimeta 177.5.

Wanawake wafupi walihesabika kuwa na urefu chini ya sentimeta 153 wakati wanawake warefu walikuwa na urefu wa sentimeta 166.4.

Kwa kuwa watu wafupi huwa na mishipa midogo ya damu ya coronary artery, hali hiyo huchangia kuwafanya wawe kwenye nafasi kubwa ya kukumbwa na matatizo ya msukumo wa damu mwilini.

Matokeo ya utafiti huu yalitolewa kwenye jarida la European Heart Journal baada ya kuwashirikisha jumla ya watu milioni 3.

Dr Tuula Paajanen, wa chuo kikuu cha Tampere nchini Finland, aliyeongoza utafiti huo alisema kuwa kwa miaka mingi kumekuwa na mjadala mrefu kuhusiana na urefu wa mtu kuwa mojawapo ya sababu za kupata magonjwa ya moyo.

Dr Paajanen alisema kuwa matokeo ya utafiti huu yanaonyesha kuwa ufupi wa mtu ni sababu inayojitegemea ya mtu kupata magonjwa ya moyo.

Dr Paajanen alisema kuwa mbali ya unene, uzee na kiwango kikubwa cha kolestro, ufupi nao inabidi uongezwe katika sababu zinazochangia matatizo ya moyo.


source nifahamishe

Imamu Mwanamke Anapowasalisha Wanaume

Sunday, June 13, 2010 / Posted by ishak / comments (0)



Mwanamama wa Kanada Raheel Raza kama ilivyotarajiwa jana aliweka rekodi kwa kuwa mwanamke wa kwanza wa kiislamu nchini Uingereza kusalisha sala ya ijumaa. Raheel aliwaambia waumini waliokuwepo msikitini kuwa si dhambi katika uislamu mwanamke kusalisha wanaume.
Mwandishi wa habari wa Kanada ambaye pia mwanaharakati wa kupigania usawa wa kijinsia katika dini ya kiislamu, Raheel Raza jana aliweka rekodi ya kuwa imamu mwanamke wa kwanza nchini Uingereza.

"Nilikuwa mwanamke wa kwanza kuwa imamu nchini Kanada, mwanamke kusalisha wanaume si dhambi, hata mtume wetu ametoa ruhusa ingawa baadhi ya maimamu wanakubali na wengine wanaona si sahihi ni makosa", alisema Rahel.

"Mimi kabla ya kutoa uamuzi wangu nilifanya utafiti na nimegundua kuwa ni sahihi na hamna kosa lolote".

"Nimetumiwa email nyingi za vitisho vya kuuliwa ili nisirudie tena kuwa imamu, hata hivyo mimi uimamu sio kazi yangu, nimekuja hapa baada ya kuitwa na watu", alisema Rahel.

Naye kiongozi wa kituo cha waislamu cha Oxford, Dr. Taj Hargey, ambaye ndiye aliyemualika Rahel kuja kusalisha katika kituo chao, alisema kuwa wanawake kuongoza misikiti si suala la kujadili.

"Hakuna aya katika Quran inayokataza wanawake kusalisha au kuongoza misikiti, katika uislamu wanaume na wanawake ni sawa. Kama katika misikiti hakuna usawa wa jinsia basi katika jamii pia hakutakuwa na usawa", alisema.

"Huenda ikawa ni vigumu kuwa na imamu mwanamke nchini Saudi Arabia au Pakistan lakini haimanishi kuwa ni makosa kuwepo sehemu zingine", aliongeza Dr. Taj Hargey.

Dr. Taj Hargey alisema kuwa sala ya jana haikukumbana na vipingamizi vyovyote hivyo inamaanisha kuwa watu wanaanza kuelewa na kukubali taratibu taratibu.

"Inabidi turudie kufanya hivi mara nyingi ili watu wazoee", alisema Dr. Taj Hargey

source nifahamishe

Hatimaye Sio Mungu Tena..

Sunday, June 13, 2010 / Posted by ishak / comments (0)


Mtoto aliyezaliwa nchini India akiwa na mikono minne na miguu minne ambaye alikuwa akiabudiwa kama mungu amepoteza uungu wake baada ya kufanyiwa operesheni kuondoa mikono na miguu iliyozidi.
Deepak Paswan, 7, alizaliwa katika sehemu za watu masikini nchini India akiwa ameungana na pacha wake kwenye tumbo. Alikuwa na miguu minne na mikono minne lakini kichwa kimoja.

Waumini wa dini ya Hindu katika kijiji chake kilichopo kwenye jimbo la Bihar walikuwa wakimtembelea nyumbani kwake wakimuabudu kama Mungu wa Kihindu anayeitwa Vishnu.

Familia yake haikufurahia jinsi mamia ya watu walivyokuwa wakienda nyumbani kwao kwaajili ya kumuabudu mtoto huyo na waliomba msaada kwa watu ili mtoto huyo afanyiwe upasuaji.

Hatimaye maombi yao yalikubaliwa mei 30 mwaka huu na hospitali moja katika mji wa Bangalore ilikubali kulipa gharama zote za kumfanyia operesheni mtoto huyo.

Baada ya operesheni ngumu ya masaa manne, madaktari walifanikiwa kuondoa viungo vilivyozidi toka kwenye mwili wa mtoto huyo.

Deepak akitambulishwa mbele ya waandishi wa habari, alionekana kufurahia hali yake mpya ambayo imempotezea sifa yake ya uungu ambayo waumini wa Hindu walimpa.

"Siku zote tulitaka afanyiwe operesheni ili atenganishwe na pacha wake aliyejiunga tumboni mwake ili kuepuka watu kumfanya mtoto wetu chombo cha ibada", alisema baba wa mtoto huyo Viresh Paswan.

"Hatimaye ndoto yangu imetimia sasa tutafanya sherehe tutakaporudi kijijini kwetu", alisema Paswan.

source nifahamishe