Afisa Magereza Atupwa Jela Kwa Kufanya Mapenzi na Mfungwa

Friday, January 29, 2010 / Posted by ishak / comments (0)


Afisa magereza mwanamke wa jela moja nchini Uingereza amehukumiwa kwenda jela miezi 21 baada ya kupatikana na hatia ya kufanya mapenzi na mfungwa ndani ya jela.
Lisa Harris, afisa magereza katika jela ya Pentonville jijini London, amehukumiwa kwenda jela miezi 21 kwa kufanya mapenzi na mfungwa ambaye anasubiria hukumu yake kwa kula njama ya kumwagia tindikali mpenzi wake wa zamani.

Lisa alikiri makosa matatu ya kujivinjari na mfungwa huyo mwanaume wakati wa kazi ndani ya jela hiyo ya wanaume.

Lisa mwenye umri wa miaka 28 anatuhumiwa kufanya mapenzi na mfungwa hatari Daniel Lynch ambaye alitupwa jela baada ya kumtuma mtu amwagie tindikali mpenzi wake wa zamani.

Daniel alimtuma mwanaume huyo amwagie mpenzi wake wa zamani tindikali ya sulphuric acid.

Daniel pia anakabiliwa na mashtaka mengine ya kumbaka mtangazaji wa taarifa ya habari, Katie Piper.

source nifahamishe

Jambazi Lasalimisha Silaha Kigoma, Laachiwa Huru

Friday, January 29, 2010 / Posted by ishak / comments (0)


Jeshi la polisi mkoani Kigoma limemwachia huru kwa msamaha maalumu mkazi mmoja wa kijiji cha Nyamidaho wilayani Kasulu aliyesalimisha kwa serikali ya kijiji, silaha ya kivita aliyokuwa akiitumia kwa ujambazi.
Kamanda wa polisi mkoani Kigoma kamishina msaidizi wa polisi George Mayunga amemtaja mtu huyo kuwa ni Nathan Morton aliyekuwa akitajwa kuimiliki silaha hiyo kinyume cha sheria.

Kamanda Mayunga ameeleza kuwa, Morton amejisalimisha kwa mwenyekiti wa kijiji Bw. Henriko Kimorimori baada ya ushawishi mkubwa uliomtaka kujisalimisha kabla ya jeshi la polisi kufanya msako.

Amebainisha kuwa bunduki iliyokamatwa ni SMG yenye namba za usajili 109484 na kwamba jeshi la polisi kwa kutambua umuhimu wa mtu kusalimisha mwenyewe limempa msamaha na kipindi cha matazamio.

Aidha katika tukio hilo lililotokea ijumaa iliyopita, serikali ya kata ya Nyamidaho imeagizwa kuunda timu maalumu itakayofuatilia mwenendo wa maisha ya Bw. Nathan Morton ili kuhakiki kama hajihusishi na uharifu zaidi.

Kufuatia tukio hilo mkuu wa polisi mkoa wa Kigoma George Mayunga ametangaza rasmi kutoa msamaha kwa jambazi atakayesalimisha silaha kwa hiyari katika kipindi cha mwezi mmoja.

Amesema endapo mmiliki haramu wa silaha atajisalimisha jeshi la polisi halitamchukulia hatua yoyote zaidi ya kumpa ushauri nasaha wa kubadili tabia na kuacha uhalifu.

Hata hivyo kamanda wa polisi mkoa wa Kigoma amesisitiza kuwa operesheni kamambe inaendelea ili kuhakikisha wamiliki wa silaha na watekelezaji wa vitendo vya ujambazi wanakamatwa na kufikishwa katika mkondo wa sheria.

Na katika tukio jingine lisilo la kawaida, mkazi mmoja wa manspaa ya kigoma Ujiji Bw. Hassan Baguma anashikiliwa na jeshi la polisi baada ya kukamatwa wakati akifanya shambulio la hatari kwa kuwakata kwa panga mkewe, shemejiwe na mama mkwe wake.

Tukio hilo limetokea jumanne wiki hii katika mtaa wa hali ya hewa mjini Kigoma umbali wa mita 200 toka makao makuu ya polisi Kigoma wakati Bw. Hassan alipofika ukweni kwake na kuanza kuwashambulia wana ndugu hao kwa mapanga na kuwajeruhi vibaya.

Kamanda George Mayunga amewataja waliojeruhiwa kuwa ni mke wa mtuhumiwa Bi.Mwamini Francis, Shemejie aliyetambuliwa kwa jina la Emanuel Baguma na mama mkwe wake ajulikanaye kwa jina la Asia Francis.

Majeruhi wote wamelazwa katika hospitali ya mkoa wa Kigoma Maweni ambako wanaendelea kupata matibabu.

Chanzo cha Bw. Hassan kuwacharanga mapanga wanandugu hao kinatajwa kuwa ugomvi wa ndoa baina yake na mkewe Bi. Mwamini ambaye mumewe anamtuhumu kumfilisi na kisha kumkimbia na kuambatana na wanaume wengine kwa ushawishi wa mama yake na ndugu wengine.

source nifahamishe

Mtoto Aliyezaliwa Akiwa na Miguu Minne, Mikono Minne Aanza Shule

Friday, January 29, 2010 / Posted by ishak / comments (0)



Mtoto wa nchini India ambaye alizaliwa akiwa na miguu minne na mikono minne, ameanza shule miaka miwili baada ya kufanyiwa operesheni ya kuviondoa viungo vilivyozidi.
Lakshmi Tatma alichukua nafasi kubwa kwenye vyombo vya habari alipozaliwa katika mji wa Bihar nchini India miaka minne iliyopita akiwa na miguu minne na mikono minne.

Lakshmi alizaliwa mwili wake ukiwa umeungana kuanzia kiunoni na pacha mwenzake ambaye alikuwa hana kichwa na hivyo kumfanya awe na jumla ya miguu minne na mikono minne.

Wakati huo kutokana na maumbile yake ya ajabu Lakshmi alikuwa akiabudiwa kama mungu wa kihindu.

Baada ya operesheni kubwa iliyofanyika miaka miwili iliyopita ambayo ilimalizika kwa mafanikio makubwa, miguu na mikono iliyozidi kwenye kiwiliwili chake iliondolewa.

Hivi sasa Lakshmi ametimiza miaka minne na ameanza shule sambamba na watoto wenzake.

"Nikifikiria jinsi alivyokuwa, sikutegemea Lakshmi angeweza kwenda shule au angekuwa na maisha aliyo nayo sasa", alisema mama yake Poonam, mwenye umri wa miaka 26.

"Vitu vyote ambavyo anaweza kuvifanya sasa alikuwa hawezi kuvifanya kabla ya operesheni, alikuwa hawezi hata kukaa lakini sasa anaweza hata kukimbia na kucheza na watoto wenzake", aliendelea kusema mama yake.

Lakshmi pamoja na kwamba hivi sasa amepona kabisa bado anahitajika kufanyiwa operesheni zaidi baada jinsi anavyozidi kukua ili kuvirekebisha viungo vyake.


source nifahamishe

Rais wa Pakistan Huchinja Mbuzi Mweusi Kila Siku ili Asirogeke

Friday, January 29, 2010 / Posted by ishak / comments (0)


Rais wa Pakistan, Asif Ali Zardari huchinja mbuzi mweusi mmoja kila siku ndani ya nyumba yake ili kujilinda na macho ya watu wenye husda na pia kujilinda na uchawi.
Msemaji wa rais wa Pakistan ameliambia gazeti la Dawn kuwa mbuzi hao huchinjwa katika misingi ya sadaka ambapo nyama hugaiwa kwa maskini ili kujipatia baraka za mungu na kuepukana na mabalaa.

"Umekuwa ni utaratibu wa kawaida wa Zardari kutoa sadaka ya nyama ya mbuzi. Amekuwa akifanya hivi kwa muda mrefu sana", alisema msemaji huyo wa rais, bwana Farhatullah Babar.

Mamia ya mbuzi wameishachinjwa ndani ya nyumba ya Zardari tangia alipoapishwa kuwa rais wa Pakistan mwezi septemba mwaka 2008, liliripoti gazeti la Dawn.

Inasemakana kuwa Zardari amekuwa akifanya hivyo kutokana na mambo kutomwendea vizuri katika uongozi wake.

Zardari aliingia madarakani baada ya kuuliwa kwa mkewe, waziri mkuu wa zamani wa Pakistan, Benazir Bhutto mwishoni mwa mwaka 2007.

Zardari anakabiliwa na misukosuko katika uongozi wake kutokana na upinzani wa kisiasa, kutetereka kwa uchumi na pia kutokana na vita dhidi ya wanamgambo wa kiislamu wanaowasapati Taliban.

source nifahamishe

Adhana Inapopigwa Kanisani Kuwaita Waislamu..

Friday, January 29, 2010 / Posted by ishak / comments (0)


Sauti kubwa ya adhana ikitoka kanisani iliwashangaza watu wengi katika mji wa Mainz nchini Ujerumani waliokuwa hawajui nia ya msanii wa Ujerumani ambaye alitumia adhana na kengele ya kanisani kuwakusanyisha waislamu na wakristo.
Katika kuleta amani na upendo baina ya waislamu na wakristo, msanii wa Ujerumani, Miriam Kilali alitumia staili ya aina yake kuwavuta watu kwa kupiga adhana ndani ya kanisa kuwaita waislamu na kutumia kengele kuwaita wakristo.

Miriam mwenye umri wa miaka 44 alirekodi adhana kwenye radio na kwenda kuipiga kwenye spika kubwa ndani ya kanisa na kuwafanya watu wengi wapita njia na wakazi wa maeneo ya karibu na kanisa hilo wabaki wakishangaa imekuwaje adhana inasikika kutokea kanisani.

Adhana ya kwanza ilisikika leo ijumaa saa nane mchana kwa saa za Ujerumani kabla ya kufuatiwa na milio ya kengele inayotumika siku zote kuwaita watu kanisani.

Adhana ilisikika leo kwa takribani dakika sita toka kwenye kanisa la St Anthony Chapel katika mji wa Mainz na itasikika tena siku ya jumamosi saa nne asubuhi, saa nane mchana na saa 11 jioni.

"Hii haikubaliki", alilalamika mwanamama mmoja wa kijerumani ambaye hakutaka kutaja jina lake.

"Wamechukua kila kitu chetu... zamani tulikuwa nchi ya kikatoliki", aliendelea kulalama mwanamama huyo.

"Najihisi kama nipo nyumbani vile ninaposikia adhana kama hii", alisema Mturuki Asil Yenertürk (52) akikumbushia adhana nchini Uturuki.

Naye mjerumani Johanna Demhardt mwenye umri wa miaka 70 alisema kuwa adhana hiyo imemkumbusha ziara yake nchini Singapore na aliendelea kusema kuwa si sahihi kwa adhana kusikika katika mitaa ya Mainz.

Naye Miriam muandaaji wa adhana hiyo kanisani alisema kuwa aliamua kufanya hivyo ili kujenga uhusiano mwema kati ya waislamu na wakristo.

"Mijadala mizito ya kujengwa misikiti barani ulaya, kuwakataza wanawake kuvaa hijab, kuwahusisha waislamu na ugaidi ni mojawapo ya mambo yanayoongeza chuki kati ya waislamu na wakristo", alisema Miriam.

Miriam alisema kuwa aliamua kutumia adhana na kengele kwa wakati mmoja ili kuwaunganisha waislamu na wakristo kwa kutumia maonyesho ya sanaa yanayoendelea kwenye kanisa hilo.

source nifahamishe

Wachina ni NOMA kwa Kukopi - Wavumbua Goojle Badala ya Google

Friday, January 29, 2010 / Posted by ishak / comments (0)


Wachina wamedhihirisha kwa mara nyingine kuwa wao ni wakali wa kukopi kwa kuikopi tovuti ya google na kutoa tovuti yao inayoitwa Goojle na pia kwa kuikopi YouTube na kutoa YouTubecn.
Wachina katika kuendeleza mpambano na tovuti za kampuni ya Google ya Marekani wameziigiza tovuti za Google na YouTube.com na kutoa tovuti zao za Goojle na YouTubecn.com.

Hivi karibuni Google walitishia kusimamisha shughuli zao nchini China kutokana na mashambulizi toka kwa hackers wa nchini China.

Katika kuendeleza vita hivyo, Wachina wametoa tovuti ya Goojle ambayo imetengenezwa kwa kuigiza kila kitu kutoka kwenye Google. Kuanzia rangi mpaka mpangilio wa ukurasa wa Google.

Herufi "jle" katika Goojle zinamaanisha dada kwa lugha ya taifa ya China, Mandarin wakati herufi "gle" katika Google zinamaanisha kaka katika lugha ya Kichina.

Tovuti ya Goojle imeambatanisha meseji ambayo inasema "Dada alikuwa na furaha sana baada ya kaka kuutupilia mbali uamuzi wake wa kuondoka na kuamua kukaa na dada yake". Meseji hiyo ilikuwa ni kijembe kwa Google ambao wanatishia kusimamisha shughuli zao nchini China.

Nayo YouTube ya Kichina YouTubecn.com video zake zote zinatoka kwenye YouTube original inayomilikiwa na Google ambayo imepigwa marufuku nchini China.

Tovuti hizo mbili ziliwekwa online kuanzia katikati ya mwezi huu punde baada ya google kutishia kusimamisha shughuli zake nchini China.

Kampuni ya Google yenye makazi yake mjini California ilifungua matawi yake nchini China mwaka 2006 na ilisema kuwa itaendelea kuwepo nchini China iwapo serikali ya China itasaidia kukomesha mashambulizi ya hackers wa China.

Wachina ni maarufu kwa kutoa bidhaa feki kuanzia kwenye magari mpaka kwenye madawa. Tovuti ya Goojle ni kithibitisho kuwa Wachina wanatisha kwa kutoa vitu vya kukopi.


source nifahamishe

Serikali kugharimia wanafunzi mitihani

Tuesday, January 26, 2010 / Posted by ishak / comments (0)

SERIKALI itatumia takribani Sh bilioni 20 mwaka ujao wa fedha kuendesha shughuli za mitihani baada ya kutangaza uamuzi wa kufuta ada ya mitihani ambayo ilikuwa ikigharimia shughuli hizo.

Uamuzi wa Serikali kubeba mzigo huo wa gharama, umetokana na kile kilichoelezwa jana na Naibu Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Mwantumu Mahiza, kuwa ni kubaini kwamba maelfu ya wanafunzi walikuwa wakishindwa kufanya mitihani baada ya kukosa ada au fedha zao kutowasilishwa na wakuu wa shule.

Akizungumza na gazeti hili jana mjini hapa, Mahiza alisema kulingana na takwimu zilizopo za wanafunzi walioshindwa kufanya mitihani katika miaka ya nyuma, endapo uamuzi wa kufuta ada usingechukuliwa, zaidi ya wanafunzi 50,000 wa shule za Serikali wasingefanya mitihani.

“Miaka ya nyuma tumepoteza maelfu ya wanafunzi. Tusipofanya hivi zaidi ya wanafunzi 50,000 watapotea,” alisema.

Pamoja na Serikali kuamua kubeba jukumu hilo, Mahiza alisema Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Profesa Jumanne Maghembe, ameagiza wanafunzi 29,000 wa kidato cha pili walioshindwa kufanya mtihani mwaka jana kwa kukosa ada, watafutwe na uandaliwe utaratibu utakaowawezesha kurudi shuleni. Amewaagiza wakaguzi kuanzia Februari mosi hadi 12 mwaka huu, wawaandalie utaratibu.

Mahiza ambaye alikuwa akizungumzia yaliyojiri katika mkutano wa watendaji wa kitaaluma ambako Waziri Maghembe alitamka uamuzi wa kufuta ada za mitihani, aliweka bayana takwimu za idadi ya wanafunzi walioshindwa kufanya mitihani tangu mwaka 2007 hadi mwaka jana.

Alisema mwaka 2007, wanafunzi 25,310 wa kidato cha pili hawakufanya mtihani; 3,870 kidato cha nne na 351 cha sita.

Mwaka juzi, ambao hawakufanya mtihani ni 17,970 cha pili, 3,500 cha nne na 251 cha sita.
Wanafunzi ambao hawakufanya mtihani mwaka jana ni 29,700 kidato cha pili, 3,500 cha nne. Kwa upande wa kidato cha sita, idadi haijajulikana kutokana na kwamba wanatarajiwa kufanya mtihani wiki ya pili ya mwezi ujao.

“Agizo hili haliwahusu wa kidato cha sita na hawawezi kurudishiwa ada walizotoa,” alisema Naibu Waziri.

Kwa mujibu wa Mahiza, Kanda ya Ziwa inaongoza kwa kuwa na wanafunzi 8,000 wa kidato cha pili ambao hawakufanya mtihani wa kidato cha pili. Inafuatia Kanda ya Magharibi yenye wanafunzi 7,000.

Akielezea uamuzi wa kufuta ada hizo mwaka huu, Mahiza alisema dhamira ya kufanya hivyo ilianza mwaka 2007 walipobaini hali ilivyo.

Alisema lakini Serikali ilichelea kuchukua uamuzi kutokana na madeni mengi iliyokuwa ikidaiwa na walimu na wazabuni waliokuwa wakisambaza chakula katika shule na vyuo.

“Mwaka juzi tukaona bado kuna mzigo mkubwa. Ilipofika mwaka jana, tukaona kwamba kuna ahueni. Lakini tulichelewa kuingiza kwenye bajeti.“Mwaka huu sasa wizara haina mzigo mkubwa, madai yamelipwa na suala la chakula ni jukumu la Tamisemi (Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa),” alisema Mahiza.

Kuhusu mambo mengine yaliyojadiliwa katika mkutano huo uliohusisha maofisa elimu, wakaguzi na wakuza mitaala, maofisa mitihani na watafiti, Mahiza alisema ni chimbuko la kushuka kwa ufaulu wa wanafunzi.

“Utafiti umebaini kuna mambo mengi yanachangia, lakini kubwa ni uwajibikaji mdogo,” alisema. Alitoa mfano kwamba utafiti, ukiwamo wa Wizara uliofanywa tangu mwaka 2007 hadi mwaka juzi, ulibaini, kwamba walimu hawakamilishi mada zinazostahili kufundishwa, mahudhurio mabaya ya wanafunzi, uhaba wa walimu na vifaa vya kufundishia na kujifunzia ni mambo yanayochangia tatizo.

Kupitia mkutano huo, halmashauri zote zimeagizwa kuhakikisha zinafufua mfumo wa kutoa mafunzo kazini kupitia vituo vya mafunzo. Mitaala ya vyuo vya ualimu, hususan ya Hisabati, Kiingereza na Sayansi pia itaboreshwa.

Naibu Waziri aliliambia gazeti hili kwamba yapo mambo mengi yaliyozungumzwa kwenye mkutano huo kwa ajili ya kuboresha elimu nchini na kwamba umeandaliwa waraka utakaomwezesha Waziri Maghembe kutoa tamko rasmi juu ya yote yaliyojiri.

Katika hatua nyingine, Mahiza akijibu swali bungeni, alisema kamwe suala la madeni ya walimu halitakuwa tishio au fimbo dhidi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), katika Uchaguzi Mkuu ujao kwa kuwa linashughulikiwa ipasavyo.

Mahiza alikuwa akijibu swali la nyongeza, la Mbunge wa Meatu, Salum Khamis Salum (CCM), aliyetaka kujua ni lini mchakato wa kuhakiki madai yote ya walimu utakamilika rasmi na kuitaka Serikali itoe jibu kamili kwa kuwa mwaka huu ni wa uchaguzi na Chama cha Walimu Tanzania (CWT) kinaweza kutumia ‘fimbo’ hiyo dhidi ya CCM.

Alisema walimu ni sehemu ya watumishi wa umma na wanaongozwa na taratibu na kanuni za utumishi wa umma, kutokana na hali hiyo, mchakato huo wa kuhakiki ni endelevu ili kila mtu apate haki yake.

“Kwa hili hakuna tishio la CWT kwa CCM hii ni haki yao kama watumishi kwa wale wanaostahili na CCM itashinda,” alisema Mahiza huku akishangiliwa na wabunge wa CCM.

Awali akijibu swali la msingi la Mbunge wa Mtambile, Masoud Abdallah Salim (CUF), ambaye alitaka kufahamu ni walimu wangapi wamelipwa hadi sasa, Mahiza alisema baada ya kukamilika kwa mchakato wa uhakiki wa madeni ya walimu Februari mwaka jana, walimu 61,423 walilipwa huku 14,215 madai yao yakikataliwa.

Alisema walimu ambao madai yao yalikataliwa ni kutokana na kutofuata taratibu, kughushi nyaraka na kukosa vielelezo.

source habari leo

Kuelekea uchaguzi mkuu: Idadi ya wabunge kuongezwa

Tuesday, January 26, 2010 / Posted by ishak / comments (0)


HATIMAYE Tume ya Taifa ya Uchaguzi (Nec) imetangaza mpango ambao utaweza kuondoa misuguano ndani ya vyama kwenye baadhi ya majimbo baada ya kueleza uwezekano wa kuongeza idadi ya majimbo ya uchaguzi kabla ya uchaguzi mkuu uliopangwa kufanyika Oktoba 25.

Tayari misuguano imeshaanza kuonekana kwenye baadhi ya vyama, na hasa tawala kutokana na wanachama wake kutangaza nia yao ya kuwania ubunge kwenye majimbo ambayo kwa sasa yanashikiliwa na wabunge kutoka chama chao, hali inayoashiria uwezekano wa kuwepo na vita kali ya ubunge.

Lakini Nec jana ilitangaza kuwa itafanya uchunguzi kuona kama kuna haja ya kuongeza majimbo kabla ya uchaguzi mkuu ujao kama sheria inavyoipa tume hiyo mamlaka ya kugawa majimbo kila baada ya miaka kumi.

Bunge la sasa la Jamhuri ya Muungano lina wabunge 323 ambao wakiingia kwenye ukumbi wao mjini Dodoma ambao una uwezo wa kuchukua watu 346, kunakuwa na upungufu wa watu 23.

Mbali na kutangaza nia hiyo ya kuongeza idadi ya majimbo, Nec jana iliweka wazi kwamba mchakato mzima wa uchaguzi huo, utagharimu Sh64 bilioni.

Makamu mwenyekiti wa Nec, Jaji Omar Makungu alisema jana kuwa majimbo hayo yataongezwa kwa mujibu wa sheria ya mwaka 1977 ambayo imeipa tume hiyo mamlaka ya kuchunguza mipaka na kugawa majimbo kila baada ya miaka kumi.

"Kwa mujibu wa katiba ya Tanzania ya 1977, Nec imepewa mamlaka ya kuchunguza mipaka na kuigawa katika maeneo mbalimbali kwa ajili ya uchaguzi wa wabunge," alisema alipozungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam.

"Aidha kwa mujibu wa katiba hiyo, tume inatakiwa kufanya uchunguzi wa mipaka na kugawa majimbo mara kwa mara au angalau kila baada ya miaka kumi."

Alisema: "Kwa kuzingatia matakwa hayo, Nec inatarajia kufanya uchunguzi wa mipaka ya majimbo ya uchaguzi na kugawa majimbo kama itahitajika kabla ya uchaguzi mkuu ujao."

Jaji alitaja vigezo 12 vitakavyotumika kugawa majimbo hayo kuwa ni pamoja na mawasiliano, hali ya kijiografia, idadi ya watu, idadi ya watu ambayo inatokana na makasio ya ongezeko la watu hadi mwaka 2008 na inayotokana na sensa ya mwaka 2002.

"Mgawanyo wa wastani wa idadi ya watu ndiyo kigezo kikuu na cha kwanza katika kuamua majimbo gani yagawanywe. Takwimu za idadi ya watu zitakazotumika zimepatikana kutoka Ofisi ya Taifa ya Takwimu," alisema Jaji Makungu.

"Pia idadi ya watu katika jimbo inapatikana kwa kuchukua idadi ya watu wote nchi nzima kugawanya kwa idadi ya majimbo yaliyopo ambayo ni 232. Ambapo idadi ya watu katika majimbo ya uchaguzi vijijini ni 206,130 na mijini ni 237,937."

Vigezo vingine ni hali ya kiuchumi ambacho hutumia ukusanyaji wa mapato katika eneo husika.

"Hapa uangalifu utachukuliwa ili maeneo ambayo yako juu sana kiuchumi yasimeze kiuwakilishi maeneo yaliyo chini kiuchumi. maeneo yaliyochini kiuchumi yatafikiriwa," alisema.

Vigezo vingine ni ukubwa wa eneo la jimbo, mipaka ya kiutawala, jimbo moja lisiwe ndani ya wilaya ua halmashauri mbili, kata moja isiwe ndani ya majimbo mawili ya uchaguzi.

Vingine ni mpangilio wa maeneo ya makazi ya watu yaliyopo, mazingira ya Muungano baina ya Bara na Visiwani, uwezo wa ukumbi wa Bunge pamoja na viti maalum vya wanawake.

"Katiba imetenga kiasi kisichopungua asilimia 30 kwa ajili ya wabunge wanawake wa viti maalum ili kuweka usawa wa kijinsia japokuwa kiwango hicho kinaweza kuongezeka," alisema.

Jaji Makungu alisema maombi, maoni na mapendekezo ya kugawa kwa majimbo au kuchuguza yanatakiwa yawasilishwe kwa mkurugenzi wa halmashauri husika na yatajadiliwa katika vikao rasmi.

"Mwisho wa NEC kupokea maombi ni Februari 28 mwaka huu na tutafanya uchambuzi kisha mashauriano na halmashauri husika kabla ya kufikia uamuzi. Tume inatarajia kukamilisha zoezi hili mwezi Aprili," alisema.

Katibu wa Bunge Dk Thomas Kashillilah aliliambia gazeti hili baadaye jana kuwa Bunge lina uwezo wa kuchukua wabunge 346 tu kwa wakati mmoja. Kwa sasa Bunge lina wabunge 323.

"Ukumbi wa Bunge letu una uwezo wa kubeba watu 346 tu sasa kuna wabunge 323," alisema Dk Kashillilah alipoulizwa na gazeti hili kufafanua suala hilo.

Akizungumzia katika mkutano huo wa waandishi wa habari mkurugenzi wa Uchaguzi Rajab Kiravu alisema kazi ya kuchunguza mipaka na ugawaji wa majimbo hayo itagharimu Sh50 milioni.

Kiravu alisema gharama zote za mchakato wa uchaguzi huo zitakuwa Sh64 bilioni ikiwa ni nyongeza ya Sh3 bilioni ikilinganishwa na gharama zilizotumika katika uchaguzi wa mwaka 2005.


source mwananchi

Madaktari Waukata Mguu wa Kushoto Badala ya Mguu wa Kulia

Tuesday, January 26, 2010 / Posted by ishak / comments (0)




Wednesday, January 27, 2010 12:42 AM
Madaktari nchini Peru bila kutarajia waliukata mguu wenye afya badala ya mguu uliotakiwa kukatwa wenye maambukizi na walipogundua kosa lao waliumalizia kuukata mguu uliobaki hivyo kumwacha mgonjwa akiwa amepoteza miguu yake yote miwili.
Madaktari nchini Peru walijichanganya na kuukata mguu wa kushoto wa mwanaume mwenye umri wa miaka 86 badala ya kuukata mguu wake wa kulia ambao ulikuwa na maambukizi.

Mwanaume huyo alitakiwa kukatwa mguu wake wa kulia ili kuzuia maambukizi katika mguu wake kusambaa mwilini mwake.

"Nilishtuka sana niliponyanyua shuka na kuona madaktari wameukata mguu wake wa kushoto badala ya mguu wa kulia", alisema binti wa mwanaume huyo, Carmen Villanueva.

Carmen alisema kuwa madaktari katika mji wa Callao walikuwa wakimpatia matibabu baba yake tangia januri 4 mwaka huu kutokana na maambukizi aliyokuwa nayo katika mguu wake wa kulia.

Baada ya hali yake kuwa mbaya sana siku ya jumamosi, waliamua kufanya operesheni ya dharura kuukata mguu huo ili kuzuia maambukizi kusambaa mwilini mwake.

Baada ya kugundua makosa yao, madaktari waliamua kumfanyia operesheni nyingine mwanaume huyo siku iliyofuatia na kuukata mguu wake wa kulia uliotakikana kukatwa tangia awali na kumwacha mwanaume huyo akiwa amepoteza miguu yake yote miwili bila kutegemea.

Hospitali ya Sabogal Hospital ilisema imewasimamisha kazi kwa muda madaktari waliofanya operesheni hizo huku uchunguzi wa tukio hilo ukiendelea.

Waziri wa afya wa Peru, Oscar Ugarte alithibitisha tukio hilo na kusema "Bila shaka wanastahili kuadhibiwa.. ni tukio la kusikitisha na tumeanzisha uchunguzi".

Familia ya mwanaume huyo imepanga kufungua kesi mahakamani kuwashataki madaktari hao.


source nifahamishe

Haiti Yakabiliwa na Ukata wa Makaburi

Tuesday, January 26, 2010 / Posted by ishak / comments (0)


Kufuatia tetemeko kubwa ka ardhi lililoikumba Haiti wiki mbili zilizopita, Haiti hivi sasa inakabiliwa na uhahaba wa makaburi ya kuwazika maelfu ya watu waliofariki kutokana na tetemeko hilo la ardhi.
Tetemeko kubwa ka ardhi la ukubwa wa 7.0 lililoikumba Haiti wiki mbili zilizopita, limesababisha uhaba wa makaburi ya kuwazika maelfu ya watu waliofariki kutokana na tetemeko hilo.

Watu zaidi ya 150,000 wanahofiwa kufariki kwenye tetemeko hilo la ardhi.

Mamia ya watu wamezikwa kwenye makaburi ya pamoja lakini bado idadi kubwa ya maiti zimezagaa kwenye mitaa ya mji mkuu wa nchi hiyo Port au Prince.

Maafisa wa shughuli za mazishi wamesema kuwa wamekuwa wakiwazika watu watatu watatu katika kila kaburi moja.

Mamia ya maiti zingine ambazo zimezagaa mitaani inasemaka zimekuwa zikichomwa moto.

Idadi kamili ya watu waliofariki kutokana na tetemeko hilo la ardhi imekuwa ni vigumu kupatikana kutokana na ugumu uliopo katika zoezi la kuhesabu miili ya watu waliofariki.

Mamia ya watu waliofariki kutokana na tetemeko hilo, miili yao bado imefunikwa kwenye vifusi vya majengo yao huku zoezi la kuokoa watu waliofunikwa na vifusi likiwa limeishasitishwa.


source nifahamishe

Kucharazwa Bakora 101 Kwa Kupata Ujazito Baada ya Kubakwa

Tuesday, January 26, 2010 / Posted by ishak / comments (0)


Msichana mwenye umri wa miaka 16 wa nchini Bangladesh amehukumiwa kucharazwa bakora 101 kutokana na ujauzito alioupata baada ya kubakwa.
Msichana mwenye umri wa miaka 16 wa nchini Bangladesh ambaye alipata mimba baada ya kubakwa, amekuhumiwa kucharazwa bakora 101.

Baba wa msichana huyo naye amepigwa faini ya pesa na pia ameonywa kuwa asipolipa faini basi familia yake itafukuzwa kwenye kijiji wanachoishi.

Taarifa zilizotolewa na wanaharakati wa kutetea haki za binadamu zilisema kuwa msichana huyo baada ya kubakwa na mwanaume mwenye umri wa miaka 20, hakuripoti tukio hilo sehemu yoyote kwa kuhofia aibu ya kubakwa.

Baada ya tukio hilo, msichana huyo aliozeshwa haraka haraka kwa mwanaume mwingine lakini alipewa talaka wiki chache baadae baada ya kugundulika kuwa ni mjamzito.

Tukio la kubakwa kwa msichana huyo lilitokea kwenye wilaya ya Brahmanbaria mwezi aprili mwaka jana.

Kwa mujibu wa gazeti la kila siku la Bangladesh, Daily Star, msichana huyo ambaye jina lake liliwekwa kapuni, aliona aibu sana kuripoti polisi kuwa amebakwa.

Kesi yake ilibumburuka hadharani baada ya wazee wa kiislamu wa kijiji hicho kupitisha hukumu hiyo na kutaka msichana huyo atengwe mpaka wazazi wake watakapokubali adhabu hiyo itekelezwe.

Mbakaji wake alikamatwa lakini alisamehewa baada ya kuomba msamaha mbele ya wazee wa kijiji.

"Nataka haki itendeke, ameniharibia maisha yangu", alinukuliwa msichana huyo akiliambia gazeti la Daily Star.


source nifahamishe

Mwanaume Mwingine Apata Mimba, Kujifungua Mwezi Ujao

Tuesday, January 26, 2010 / Posted by ishak / comments (0)


Mwanaume wa nchini Marekani ambaye alizaliwa kama mwanamke kabla ya kubadili jinsia yake kuwa mwanaume anatarajia kujifungua mtoto wa kiume mwezi ujao.
Scott Moore mwanaume wa nchini Marekani ambaye alizaliwa kama mwanamke anatarajia kuwa mwanaume wa pili wa nchini Marekani kupata mimba na kujifungua mtoto.

Scott anatarajia kujifungua mtoto wa kiume mwezi ujao.

Mume wa Scott ambaye naye alizaliwa mwanamke kabla ya kubadilisha jinsia na kubadilisha nyeti zake, anatarajia kuwa pembeni ya Scott wakati wa kujifungua.

Scott amejibadilisha jinsia kuwa mwanaume lakini alikubaliwa kuolewa kisheria na Thomas kwa kutumia cheti chake cha kuzaliwa ambacho kinamuonyesha kuwa yeye ni mwanamke.

Thomas yeye anahesabika mwanaume kwakuwa alibadilisha jinsia yake na kufanya operesheni ya kuuondoa uke na kuupandikiza uume.

Scott yeye bado hajafanya operesheni hiyo ya kuuondoa uke wake hivyo bado ana sehemu za siri za kike.

"Tunajua watu watatukosoa lakini sisi tuna furaha ya kupata mtoto na wala hatujisikii vibaya", alisema Scott mwenye umri wa miaka 30 ambaye alisema mtoto wao wamepanga kumpa jina la Miles.

Scott anasema kwamba alizaliwa kama mwanamke akipewa jina la Jessica na alianza kupata shauku ya kuwa mwanaume alipoanza kupevuka alipokuwa na umri wa miaka 11.

Scott aliendelea kusema kuwa wazazi wake awali walimpinga lakini baadae walimsaidia kutimiza nia yake ya kuwa mwanaume.

Alianza kumeza vidonge vya homoni za kiume alipokuwa na umri wa miaka 16 na wazazi wake walimlipia gharama za kuyaondoa matiti yake.

Scott anasema kuwa alishindwa kulipia gharama za operesheni ya kuutoa uke wake na kuupandikiza uume hivyo hadi leo bado ana sehemu za siri za kike.

Thomas kwa upande wake yeye alifanikiwa kufanya operesheni ya kuuondoa uke na kuupandikiza uume mwaka jana.

Scott alipata ujauzito baada ya kupandikizwa mbegu za kiume za mwanaume ambaye yuko karibu na familia hiyo.

Scott anasema kuwa ana mpango wa kumzaa mtoto wake kwa njia ya asili.

"Hatukutaka kuwashtua watu watakapoona mwanaume anajitokeza kuja kujifungua", alisema Scott akielezea jinsi walivyomtafuta daktari wa kumzalisha.

Scott anasema kuwa hawakumpata kirahisi daktari huyo kwani madaktari wengi walikuwa wakikwepa kuonana naye na hata kumpa matibabu.

"Tunataka kuwaonyesha watu kuwa watu waliobadilisha jinsia nao wanaweza kuanzisha familia zilizojaa upendo na furaha", alisema Thomas.

source nifahamishe

Always bandia zakamatwa Arusha

Tuesday, January 26, 2010 / Posted by ishak / comments (0)

JESHI la Polisi mkoani Arusha limekamata shehena ya taulo bandia za wanawake ‘Always’ zenye thamani ya zaidi ya Shilingi milioni 200 ambazo hazifai kwa matumizi hayo.
Kamanda wa Polisi mkoani humo, Bw. Basilo Matei, alisema kuwa shehena hiyo ilikamatwa juzi nyumbani kwa mfanyabiashara maarufu mmoja aishio maeneo la Baraa.

Matei alisema mfanyabiashara huyo kwa sasa jina linahifadhiwa kwa sababu za kipolisi na kusema shehena hiyo ilikuwa na maboksi zaidi ya 10,000 na zinadhaniwa kuingizwa nchini kutoka nchini China na zilishasambazwa katika maeneo ya biashara kinyemela.

Matei alieleza kuwa polisi walifanikiwa kukamata Always hizo bandia baada ya kupata taarifa kutoka kwa kampuni ya Procter & Gambo Ltd ya jijini Dar es Salaam ambayo ni wakala aliyeruhusiwa kuingiza bidhaa hizo nchini.

Alisema kampuni hiyo iligundua bidhaa hizo feki kujaa sokoni kaika maeneo mengi .

Alisema bidhaa hizo zilithibitishwa kuwa ni feki baada ya kutafutwa wataalamu wa mambo ya afya ambao walibainisha kuwa bidhaa hiyo ilikuwa ni feki na zingeweza kuhatarisha afya za akina mama yakiwemo na maambukizi ya magonjwa ya zinaa pamoja na fangasi ambao ni hatari kwa afya ya uzazi.

Alisema kati ya magonjwa ambayo ambayo mwanamke angeweza dkutumia bidhaa hizo ni pamoja na UTI ambayo wadudu hushambulia mfumo wa mkojo hatimaye kwenye viungo vya ndani vya uzazi.

Alisema daktari aliyethibitisha hilo alisema kuwa athari za maambukizo hayo ni mbaya kwani huweza kuambukiza haraka na hata wakati mwingine huleta mitafaruku ndani ya familia kwani huambukiza haraka wakati wa kufanya tendo la ndoa.

source nifahamishe

Ronaldo Amvunja Pua Mchezaji Mwenzake

Tuesday, January 26, 2010 / Posted by ishak / comments (0)


Nyota wa Real Madrid, Cristiano Ronaldo aliifungia timu yake magoli mawili ya ushindi dhidi ya timu ya Malaga lakini alitolewa nje ya uwanja kwa kadi nyekundu baada ya kumvunja pua mchezaji wa Malaga.
Cristiano Ronaldo alibaki akitoa lawama zake kwa refa aliyemtupa nje ya uwanja kwa kadi nyekundu alipoivunja pua ya beki wa Malaga, Patrick Mtiliga.

Ronaldo ambaye ndiye mchezaji ghali kuliko wote duniani, aliifungia Real Madrid magoli yote mawili yaliyoipa ushindi wa mabao 2-0 katika mechi hiyo ya jumapili jioni na kulifanya pengo la pointi kati yake na Barcelona kufikia pointi tano.

Ronaldo alikuwa akikokota mpira kwenye dakika ya 70 akijaribu kumtoka Mtiliga na ndipo alipouzungusha mkono wake mara mbili na kumgonga puani Mtiliga na kupelekea kuvunjika kwa pua yake.

Kocha wa Malaga, Juan Ramon Lopez Muniz alilaani kitendo cha Ronaldo na alisema kuwa Mtiliga atatumia wiki tatu nje ya uwanja akiuguza pua yake.

Ronaldo alitoka nje ya uwanja huku akitoa lawama zake kwa refa wa mechi hiyo akisema kuwa hakustahili kadi nyekundu.

"Watu wanaojua mpira wanajua nia yangu kuwa ilikuwa ni kuwania mpira", alilama Ronadlo.

"Najua mmeona damu mmlipoangalia kwenye TV lakini ukweli ni kwamba nilikuwa nacheza mpira tu sikuwa na nia ya kumuumiza mtu yoyote", aliendelea kusema Ronaldo.

Ronaldo aliendelea kusema kuwa alimfuata Mtiliga baada ya mechi na kumuomba radhi.

source nifahamishe

Binamu wa Saddam Hussein Anyongwa

Tuesday, January 26, 2010 / Posted by ishak / comments (0)


Binamu wa rais wa zamani wa Iraq na mpambe wa karibu wa Saddam Hussein, Ali Hassan al-Majid au maarufu kama "Chemical Ali" amenyongwa leo kwa makosa ya mauji aliyofanya wakati wa utawala wa rais Saddam.
Ali Hassan al-Majid au maarufu kama "Chemical Ali" amenyongwa leo kufuatia hukumu ya kunyongwa iliyotolewa wiki iliyopita na mahakama kuu ya nchini Iraq.

"Chemical Ali" anatuhumiwa kuwaua kwa kutumia gesi za sumu zaidi ya wakurdi 5,000 mnamo mwaka 1988.

Ali alinyongwa kwa kitanzi katika staili ile ile ambayo Saddam Hussein alinyongwa miaka mitano iliyopita.

"Adhabu ya kifo ya Ali Hassan al-Majid imeishatekelezwa", alisema Ali al-Dabbagh, msemaji wa serikali ya Iraq.

Ali aliyekuwa na umri wa miaka 68 alihukumiwa kunyongwa januari 17 mwaka huu kwa makosa ya kuamuru gesi ya sumu itumike kuwaua wakurdi zaidi ya 5,000 katika mji wa Halabja karibu na mpaka wa Iran. Maafisa wengine wa serikali ya Iraq walihukumiwa vifungo vya miaka mingi jela kwa kushiriki katika mauaji hayo.

Kabla ya kuhukumiwa kunyongwa wiki iliyopita, Ali alikuwa ameishahukumiwa kunyongwa mara tatu kwa mauaji ya wakurdi kwenye miaka ya 1980 na mauaji ya waislamu wa dhehebu la Shia kwenye miaka ya 1990.

Ali alibatizwa jina la "Chemical Ali" na wakurdi ambao pia walikuwa wakimuita "Butcher of Kurdistan".

Ali alikamatwa mwaka 2003 baada ya kuangushwa kwa serikali ya Iraq na Marekani.


source nifahamishe

Agundulika Bado Yu Hai, Akiwa Ndani ya Jeneza

Tuesday, January 26, 2010 / Posted by ishak / comments (0)


Babu mmoja mwenye umri wa miaka 76 wa nchini Poland amezinduka toka kuzimu sekunde chache kabla ya misumari kupigiliwa kwenye jeneza lake.
Babu Jozef Guzy mwenye umri wa miaka 76 ambaye ni mfugaji wa nyuki, alitangazwa amefariki kutokana na shambulio la moyo akiwa karibu na mizinga yake ya nyuki katika mji wa Katowise kusini mwa Poland.

Ambulansi iliitwa baada ya babu Jozef kukumbwa na shambulio la moyo na daktari mzoefu alitangaza baada ya kumpima kuwa Jozef ameishafariki.

"Jozef alikuwa hapumui, kulikuwa hakuna mapigo ya moyo na mwili wake ulikuwa wa baridi ambazo zote hizo ni dalili za kifo", Jerzy Wisniewski, msemaji wa ambulansi katika mji huo alisema.

Masaa matatu baada ya kutangazwa amefariki, watu wa mazishi walifika kuuchukua mwili wake.

Afisa wa mazishi, Dariusz Wysluchato aliuweka mwili wake kwenye jeneza na alikuwa kwenye hatua za mwisho za kulifunga jeneza wakati mkewe Jozef alipomtaka amvue saa aliyokuwa amevaa.

Wakati afisa huyo alipokuwa akimvua saa bila kutarajia alimgusa shingoni na kuhisi Jozef bado anapumua.

"Nilimgusa kwenye mshipa mkubwa wa damu kwenye shingo na ndipo nilipogundua kuwa hajafariki. Nilimpima tena kuhakikisha hajafariki na kuanza kupiga kelele kuita watu", alisema Dariusz.

Dariusz alimuita rafiki yake ambaye alihakikisha kuwa Jozef alikuwa akitoa pumzi hafifu sana.

Ambulansi iliitwa tena na daktari yule yule aliyesema amefariki, alimpima tena na kutangaza kuwa Jozef "amerudi toka kuzimu".

Jozef alipelekwa hospitali ambapo madaktari walishindwa kugundua ugonjwa unaomsumbua pamoja na kumfanyia vipimo kadhaa.

Baada ya kupumzishwa hospitalini kwa siku kadhaa, Jozef aliruhusiwa kurudi nyumbani kwake.

Jozef anasema kuwa kitu cha kwanza alichofanya baada ya kutoka hospitali ni kumpelekea Dariusz bakuli la asali kama shukurani kwa kuokoa maisha yake.

Tukio la Jozef limetokea ikiwa ni wiki moja tu baada ya mwanaume mmoja nchini China kutangazwa amefariki baada ya kupata ajali ya pili.

Mwanaume huyo aliyetajwa kama Zhang Houming, 46, Aliwekwa monchwari hospitalini lakini aligundulika kuwa bado yupo hai akitoa pumzi hafifu sana alipowekwa ndani ya jeneza.

Alirudishwa tena hospitali lakini alifariki lisaa limoja baadae.

Familia yake katika mji wa Neijiang imefungua kesi ya madai sawa na Tsh. Milioni 270 kama fidia.

source nifahamishe

Msoma mita wa Dawasco afikishwa mahamani kwa kuomba rushwa

Tuesday, January 26, 2010 / Posted by ishak / comments (0)

MSOMA mita wa Kampuni ya kusambaza maji safi jijini Dar es Salaam (Dawasco), Chobines Mabega (38), amefikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kinonondoni, kwa tuhuma za kuomba hongo.
Mabega alisomewa mashitaka mawili na Mwendesha Mashtaka wa Taasisi ya kupambana na Kuzuia Rushwa (PCCB), Ronald Manyiri mbele ya hakimu Sundi Fimbo wa mahakama hiyo.

Manyiri alidai kuwa mtuhumiwa anakabiliwa na mashtaka mawili yote yakiwa ni ya kuomba hongo kinyume na sheria za nchi.

Akisoma hati hiyo alidai kuwa Januari 20 , mwaka huu huko eneo la Mikocheni katika Hotel ya Keys, mtuhumiwa ambaye ni mwajiriwa wa Dawasco aliomba rushwa ya shilingi milioni 1,500,000 kwa mlalamikaji kama kishawishi cha kutomchukulia hatua za kisheria kwa kuunganisha maji kinyume cha utaratibu.

Katika shtaka la pili, ilidaiwa kuwa Januari 22, katika maeneo ya Bar Blue Star, mtuhumiwa alimshawishi mtu mwingine ampatie kiasi cha shilingi 750,000 zikiwa ni sehemu ya hongo kutoka Kinabo Masawe kwa kuwa aliunganisha maji kinyume na sheria na alimtishia ampatie kiasi hicho ili aweze kumrekebishia pasipo na mamlaka kujua.

Mtuhumiwa huyo alipotakiwa kujibu mashitaka hayo alikana hakuhusika na yupo nje kwa dhamana na kesi hiyo iliahirishwa hadi Februali 16 mwaka huu.


source.nifahamishe

jumapili njema.............

Sunday, January 24, 2010 / Posted by ishak / comments (0)