Aozeshwa Kwa Baba Mkwe Wake Kwa Mahari ya Nguruwe

Friday, January 15, 2010 / Posted by ishak /


Ni kawaida kwa mwanamke barani Afrika kuolewa kwa mahari ya ng'ombe na mbuzi lakini hali ilikuwa tofauti nchini New Zealand ambapo msichana mmoja alilazimishwa kuolewa na baba mkwe wake kwa mahari ya nguruwe mmoja aliyenona.
Msichana huyo mwenye umri wa miaka 17 alijikuta akiozeshwa kwa baba mkwe wake mtarajiwa na sio mpenzi wake kama alivyotegemea baada ya mzee huyo kutoa mahari ya nguruwe na jamvi moja la thamani kubwa.

Msichana huyo alikuwa akiishi na mama yake pamoja na baba yake wa kambo ambao wote wawili wametiwa mbaroni wakikabiliwa na makosa ya kumlazimisha msichana huyo kuolewa na mzee huyo na pia kumlazimisha kufanya mapenzi na mwanaume huyo ambaye ni baba wa mpenzi wake.

Kwa mujibu wa gazeti la Sunday Star-Times la New Zealand, mama wa msichana huyo anakabiliwa pia na mashtaka ya kumshambulia binti huyo mara mbili ili akubali kuolewa na mwanaume huyo ambaye angekuwa baba mkwe wake iwapo angeolewa na mpenzi wake.

Taarifa zaidi zilisema kwamba msichana huyo alikuwa hataki kuolewa na mzee huyo lakini kutokana na makubaliano yaliyofikiwa kati ya familia hizo mbili, alilazimishwa kukubali kuolewa.

Familia yake ilikabidhiwa mahari ya nguruwe mmoja mkubwa sana aliyenona pamoja na jamvi moja la gharama.

Usiku wa harusi yake, msichana huyo alikimbia na kwenda kwa mpenzi wake ambaye ni mtoto wa mzee huyo aliyeozeshwa kwake.

Alipogundulika amejificha kwa mpenzi wake, alifuatwa na kushambuliwa na kisha kutekwa na kurudishwa kwa mume wake ili aanze kumtumikia kama mke wake.

Mama wa msichana huyo na mumewe watapandishwa kizimbani baadae mwezi huu wakikabiliwa na mashtaka sita na iwapo watapatikana na hatia wanaweza kutupwa jela miaka 14.

source.nifahamishe

0 comments:

Post a Comment