Akamatwa na Kimada, Apigwa Faini ya Nyati Wanne

Sunday, January 31, 2010 / Posted by ishak /


Mahakama ya kikabila ya nchini Malaysia imeamuaru mwanaume aliyefumaniwa na mkewe akiishi na kimada, alipe faini ya nyati wanne na nguruwe mmoja.
Mahakama ya kikabila katika jimbo la Sabah katika kisiwa cha Borneo nchini Malaysia imemuamuru mwanaume pamoja na kimada wake walipe faini ya nyati wanne na nguruwe mmoja kwa kuishi kinyumba bila kuoana.

Kwa mujibu wa gazeti la The Star la nchini Malaysia, mwanaume huyo na kimada wake walipatikana na hatia ya kuishi pamoja bila kuoana.

Mke wa mwanaume huyo, alipeleka malalamiko kwenye mahakama ya kikabila ya mji wa Penampang akisema kuwa mumewe amekuwa akiisaliti ndoa yake na kwenda kuishi pamoja na kimada huyo.

Jaji William Sampil alisema kuwa mahakama imepata ushahidi wa kutosha kumtia hatiani mwanaume huyo na kimada wake pamoja na kujitetea kwao kuwa wao ni marafiki tu.

Jaji huyo aliamuru mwanaume huyo na kimada wake walipe fidia ya nyati wanne na nguruwe mmoja pamoja na pesa taslimu sawa na dola 600.

Taarifa ya mahakama haikuweka wazi kama nyati hao wanatakiwa kutolewa wakiwa hai au la.

Utawala wa kikabila unachukua asilimia moja tu ya watu wote milioni 28 wa nchini Malaysia.

source nifahamishe

0 comments:

Post a Comment